CUF: Wasiotaka Serikali ya Umoja wafukuzwe

Zanzibar. Chama cha Wananchi (CUF) kimesema wanasiasa wanaojadili suala la kuendelea au kutokuendelea na Serikali ya Umoja wa Kitaifa (SUK), wanastahili kujiuzulu au kufukuzwa ndani ya vyama vyao.

Kauli hiyo imekuja siku moja baada ya Mnadhimu wa Baraza la Wawakilishi Zanzibar (BLW), Salmin Awadh Salmin kusema kuwa Wawakilishi wa CCM wanajiandaa kuwasilisha hoja binafsi kwenye Baraza hilo ili kuwapa nafasi wananchi waulizwe iwapo wanataka kuendelea na Serikali ya Umoja wa Kitaifa au vinginevyo.

Salmin aliyasema hayo juzi kwenye mkutano wa hadhara uliofanyika kwenye Viwanja vya Kibandamaiti, Unguja kwa kuwa wanaona kwamba lengo la kuundwa kwake halina dalili njema kwa siku za usoni.

Jana, Mkurugenzi wa Haki za Binadamu na Mawasiliano ya Umma wa CUF, Salum Abdallah Bimani alisema: “Kimsingi mpango huo unakwenda kinyume na uamuzi wa vyama vya CCM na CUF ambao ulipitishwa na kuridhiwa na vikao vya juu vya vyama hivyo viongozi wanaopinga jambo hilo wanaonyesha kupingana na uamuzi wa vyama vyao.”

Ajenda ya siri

Mkurugenzi huyo wa CUF alikana chama chake kuwa na ajenda ya siri ya kuvunja Muungano au kuyasambaratisha Mapinduzi ya Zanzibar na kusema kinachopiganiwa ni muungano wenye usawa, haki na heshima kila upande wa washirika.

Kuhusu Ukawa kususia Bunge Maalumu la Katiba, Bimani alisema chama chake kimetoa masharti matatu yanayopaswa kuzingatiwa kabla ya kubadilisha msimamo wake. Alitaja masharti hayo kuwa ni kuijadili Rasimu ya Katiba kama iliyowasilishwa na Tume ya Mabadiliko ya Katiba; wajumbe wa CCM kuacha matusi, vijembe na ubaguzi na hilo lithibitishwe kwa maandishi na viongozi wake wa kitaifa.

Jambo la tatu ni kuhakikishiwa kuwa vikao vya Bunge vitumike kujadili rasimu na si sera za vyama vya siasa kwa vile ndiyo mwanzo wa kukaribisha malumbano na kusababisha Bunge kupoteza mwelekeo na kuweka nyufa katika Umoja wa Kitaifa.
Tags

Post a Comment

0 Comments
* Please Don't Spam Here. All the Comments are Reviewed by Admin.

Top Post Ad

Below Post Ad