KUTOKA BRAZIL: Ronaldo kivutio, lakini Balotelli zaidi Brazil

DUNIA nzima inampenda Mario Balotelli. Kuna kila supastaa wa soka  hapa nchini Brazil kwa sasa, lakini ukiondoa Neymar na wachezaji  wenzake wa timu ya taifa ya Brazil, hakuna anayefikia nyota ya Mario Balotelli.

Ndani ya ardhi ya Brazil kwa sasa kuna Cristiano Ronaldo, Lionel Messi,  Robin van Persie, Arjen Robben, Diego Costa na wengineo, lakini ukizunguka katika mitaa ya Sao Paulo, Wabrazili wanavutika zaidi  kumwangalia Balotelli. Wenyewe wanamwita ‘Maruku’ wakimaanisha kichaa.

Popote ambapo kikosi cha Italia kinapoonyeshwa katika televisheni watu wote waliopo katika baa mbalimbali za Sao Paolo wanakaa kimya na kusikiliza kinachozungumzwa kuhusu Balotelli ambaye ndiye anazungumziwa kwa muda mrefu na watangazaji.

“Tungependa kuwa na mchezaji kama yeye kikosini kwetu Brazil.  Anachangamsha timu. Unamkumbuka Edmundo? Alikuwa kama yeye.  Katika timu lazima uwe na mchezaji kichaa,” anasema dada mmoja  mhudumu wa baa ya Carcio de Italiano, Suzanne Almeda.

Mtu mmoja anajitokeza kumsifu Balotelli lakini hapo hapo anatengeneza  laana kwa Wataliano wasichukue ubingwa wa Kombe la Dunia kwa sababu wakichukua wataifikia Brazil kwa idadi ya mataji hayo.

Ikumbukwe kuwa katika fainali, Italia wamechukua mara nne  wakiifukuza Brazil ambayo imechukua mara tano. Wajerumani nao  wanaombewa dua mbaya na Wabrazili wa hapa kwa sababu wamechukua  mara tatu.

Cristiano Ronaldo anapendwa kwa sababu kubwa moja. Anatoka katika  nchi ambayo iliwatawala na kuwaachia lugha ya Kireno ambayo ni Ureno. Kwa sababu Ronaldo anazungumza lugha wanayoielewa huku  kukiwa na Wareno wengi nchini Brazil, raia wa Brazil wanamuona kama mwenzao.

Sijachunguza kwa umakini, lakini nadhani naweza kuja na mjadala huu  siku zijazo ukiendelea kusoma Mwanaspoti, nadhani Messi atakuwa  anachukiwa kwa sababu anatoka katika taifa lao pinzani, Argentina.
Tags

Post a Comment

0 Comments
* Please Don't Spam Here. All the Comments are Reviewed by Admin.

Top Post Ad

Below Post Ad