CUF Kufanya Maandamano Kesho Licha ya Jesho la Polisi Kupinga....

VIJANA wa Chama cha Wananchi kupitia jumuiya yao (JUVI-CUF) wameweka msimamo kuwa ‘iwe iwavyo’ watafanya maandamano kesho visiwani humo kwa kuwa ni haki yao kufanya hivyo licha ya Jeshi la Polisi kupinga.

Maandamano hayo yameelezwa kuwa ni sehemu kumbukumbu ya Wazanzibari waliouawa mwaka 2000 kutokana na vurugu za kisiasa zilizotokea chini ya Serikali ya Chama Cha Mapinduzi (CCM).

Maandamano hayo yametangazwa ikiwa ni siku chache baada ya Mwenyekiti wa Tume ya Uchaguzi Zanzibar (ZEC), Jecha Salim Jecha kutangaza tarehe 20 Machi mwaka huu kuwa siku ya kurudia uchaguzi visiwani humo.

Jecha alifuta matokeo ya uchaguzi mkuu visiwani humo uliofanyika tarehe 25 Oktoba mwaka jana kwa madai ya kuwepo kwa kasoro mbalimbali jambo ambalo lilipingwa na CUF, taasisi za kiraia na baadhi ya makada wa CCM.

JUVI-CUF wamepanga kufanya maandamano makubwa visiwani humo kwa lengo la kupinga dhuluma hiyo licha ya Jeshi la Polisi kuyagomea.

Wameeleza kuwa maandamano hayo watayafanya ili kuieleza dunia kwamba, Zanzibar haki inaminywa na kwamba, maandamano hayo yatakakuwa ujumbe mahsusi kwa wapenda demokrasia duniani.

Vijana hao wamesema kuwa, hawawezi kuona haki yao inapokwa na serikali kwa maslahi ya CCM na kwamba, maandamano hayo yatafanyika visiwani humo kama ilivyopangwa.

Mkurugenzi wa Habari na Mawasiliano wa JUVI-CUF, Abeid Ali amesema kuwa, wananchi wa visiwa hivyo hawatokoma kudai haki yao mpaka pale itakaposimama.

Mkurugenzi huyo ameeleza kwamba, wana imani kuwa si risasi wala mizinga ambayo inaweza kusimamisha haki visiwani humo na kwamba, watapigania haki hata kama wengine watauawa.

Kiongozi huyo amekumbushia mauaji yaliyofanywa na Serikali ya Rais Mstaafu, Benjamin Mkapa baada ya Uchaguzi Mkuu 2000 na kwamba, wananchi hawajaingia woga wala kurudi nyuma kudai haki yao.

“Sisi ni raia wakizanzibari, tuna uhuru wa kuandamana kwani CCM waliachiwa kuandamana na ulinzi wakapewa, na sisi tuna haki ya kufanya maandamano,” amesema Ali.

Amesema kuwa, maandamano hayo yatafanyika kuanzia Mtendeni kwenda Mnazimmoja na kumalizikia kwenye viwanja vya Maisara.
Tags

Post a Comment

1 Comments
* Please Don't Spam Here. All the Comments are Reviewed by Admin.
  1. Andameni tuone ccm na Polisi wao
    Wakileta bunge litanuka

    ReplyDelete

Top Post Ad

Below Post Ad