Jaji Warioba Afunguka Kuhusu Mgogoro wa Zanzibar, Adai ni Tatizo la Kikatiba

WAZIRI mkuu wa zamani, Jajji Joseph Warioba amesema tatizo lililoko Zanzibar linapaswa kutatuliwa chini ya usimamizi wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania wala sio kuachiwa vyama vinavyovutana. Anaandika Jabir Idrissa.

Jaji Warioba amesema mvutano wa vyama vya CCM na CUF unaoendelea Zanzibar kuhusiana na kufutwa kwa uchaguzi wote mkuu uliofanyika Oktoba 25, ni suala linathibitisha kuwepo kwa tatizo la kikatiba nchini.

“Tunapaswa kuliangalia tatizo la Zanzibar kikatiba zaidi kuliko kuliachia vyama vinavyovutana. Tunaliacha hivi linakuwa gumu kutatuka, lakini likiachwa hivi wananchi wanaumia,” amesema.

Jaji Warioba ametoa msimamo huo leo katika maelezo yake ya majumuisho kwenye mdahalo wa wazi uliofanyika ukumbi wa Nkrumah wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, kuhusu Uchaguzi Mkuu wa Oktoba mwaka jana.

Katika mdahalo huo, Chama Cha Mapinduzi kilitupiwa lawama kwa kutoridhia tamko la utoaji wa habari kwa usawa miongoni mwa vyombo vya habari wakati wa uchaguzi huo.

Vilevile kwenye mdahalo huo, ofisa ambaye hakutambuliwa mara moja alisema kwamba matokeo ya uchaguzi yaliyotangazwa yalitokana na matokeo yaliyokusanywa vituoni.

Amesema kwamba mfumo wa kupokelea matokeo uliotumiwa na Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC) ulikuwa wa wazi, na ambao ulitolewa kwa vyama vyote vya siasa pamoja na wadau walioshiriki uchaguzi.

Hata hivyo, alishindwa kutoa ufafanuzi kuhusu malalamiko yaliyokuwepo kwamba mfumo huo ulidhibitiwa na Tume hata baada ya baadhi ya vyama kuiomba mara kadhaa kuueleza bayana. Alisema vyama viliruhusiwa kutoa malalamiko.

Kadhalika, ofisa huyo hakusema kama ingekuwa asemalo ni kweli ilikuaje kituo cha kupokelea matokeo ya uchaguzi cha vyama vilivyo chini ya Umoja wa Katiba ya Wananchi UKAWA) kilivamiwa na Jeshi la Polisi na kuvunjwa, kompyuta kuchukuliwa na watendaji kukamatwa na kufunguliwa mashitaka mahakamani.
Tags

Post a Comment

0 Comments
* Please Don't Spam Here. All the Comments are Reviewed by Admin.

Top Post Ad

Below Post Ad