Rais Magufuli Apokea Shilingi Bilioni 12 Ya Tume Ya Uchaguzi Zilizokuwa Zimebaki Baada ya Uchaguzi Mkuu

Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC) imekabidhi shilingi Bilioni 12 kwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Pombe Magufuli, zilizobaki baada ya uchaguzi mkuu wa Madiwani, Wabunge na Rais uliofanyika tarehe 25 Oktoba, 2015.

Mwenyekiti wa Tume ya Taifa ya Uchaguzi Jaji Mstaafu Damian Lubuva amekabidhi hundi ya kiasi hicho cha fedha kwa Rais Magufuli leo tarehe 07 Juni, 2016 Ikulu Jijini    Dar es Salaam na kueleza kuwa bakaa ya fedha hizo haikuathiri kwa namna yoyote uchaguzi mkuu wa mwaka jana.

"Mheshimiwa Rais fedha ambazo tunakukabidhi, tulijibanabana sana, japo muda wenyewe ulikuwa mfupi lakini tulijibanabana sana bila kuathiri utendaji wa shughuli za uchaguzi, isije ikawa inatoa sura kwamba iliathiri, haikuathiri, na katika hali hiyo kama ambavyo wengi ni mashahidi, hatujisifii, lakini uchaguzi ulienda vizuri" Amesema Jaji Mstaafu Lubuva.

Akizungumza baada ya kupokea mfano wa hundi hiyo, Rais Dkt. John Pombe Magufuli ameipongeza Tume ya Taifa ya Uchaguzi kwa kuokoa fedha hizo na kuzirejesha serikalini ili zipangiwe majukumu mengine na ametaka taasisi nyingine za serikali ziige mfano huo wa uzalendo na kutanguliza maslahi ya taifa.

"Kitendo hiki ambacho mmekionesha leo, kinaonesha ni kwa namna gani Tume ya Taifa ya Uchaguzi chini ya uongozi wako Mheshimiwa Mwenyekiti ilivyo na watu makini na waadilifu sana, kwa sababu hizi fedha ambazo kwa lugha uliyotumia ni bakaa, kutokana na zile ambazo mlipewa zaidi ya Shilingi Bilioni 270, mkatumia shilingi Bilioni 261.6, mkabakiza shilingi Bilioni 12, mngeweza kuamua kusema hamkubakiza na hakuna mtu yeyote ambaye angewauliza, na saa nyingine pengine hakuna mtu yeyote ambaye angejua, mngeweza pia kusema kiasi mlichotupa hakijatosha, tunaomba mtuongezee ama mngetengeneza maneno mazuri mazuri ya matumizi, bado nina uhakika serikalini wasingejua" Amesema Rais Magufuli.

Pamoja na kukabidhi hundi ya bakaa ya shilingi Bilioni 12, Mwenyekiti wa Tume ya Taifa ya Uchaguzi Jaji Mstaafu Damian Lubuva amemuomba Rais Magufuli aisaidie tume hiyo kupata jengo lake la ofisi kwa kuwa hivi sasa tume inatumia majengo ya kupanga ambayo yanaigharimu tume hiyo takribani shilingi Bilioni 1 na Milioni 400 kila mwaka kwa kulipia kodi ya pango, usafiri na gharama nyingine za uendeshaji.

Rais Dkt. John Pombe Magufuli amelikubali ombi hilo na kuamua kuwa fedha ambazo Tume ya Taifa ya Uchaguzi imeziokoa (Shilingi Bilioni 12) kutoka kwenye Uchaguzi Mkuu wa Mwaka jana zitumike kujenga ofisi ya tume, na amependekeza ofisi hiyo ijengwe mkoani Dodoma.

"Na mimi ningefurahi zaidi kama hilo jengo lingejengwa Dodoma, kwa sababu Dodoma ndio makao makuu ya nchi hii, na hasa kwa sababu Dodoma ni katikati ya Tanzania" Amesisitiza Rais Magufuli.

Rais Magufuli pia amelikubali pendekezo la tume hiyo la kuanzishwa kwa mfuko wa tume ya uchaguzi ambao utakuwa unakusanya fedha kila mwaka kwa ajili ya uchaguzi mkuu unaofuata, badala ya kuendelea na utaratibu wa sasa wa kusubiri mwaka wa uchaguzi ndipo zitengwe fedha zote za kugharamia uchaguzi huo.

Gerson Msigwa
Kaimu Mkurugenzi wa Mawasiliano, IKULU
Dar es Salaam

07 Juni, 2016

Tags

Post a Comment

6 Comments
* Please Don't Spam Here. All the Comments are Reviewed by Admin.
  1. wewe acha danyanganya wadanyanyika tuna uhakika gani kwamba ni bilion 12 tu ndio zilizobaki??? nchi yenyewe imejaa mijizi watu wamezitumbua mpaka wamechoka.... kwa nini hizo ela hamkurudisha mara baada ya uchaguzi kumalizika??

    ReplyDelete
    Replies
    1. Inaonyesha unajua mengi kuhusu hizo hela,
      tuambie kuliko kuropoka.

      Delete
  2. Mmmh!Mbona zamani haikuwa hivyo?haijawahi tokea hata mara moja pesa za uchaguzi kubaki na kurudishwa,maana yake zilikuwa zinapigwa juu kwa juu AU?Ama kweli HAPA KAZI TUU.MUNGU AWANARIKI KWA KUMUUNGA MKONO JPJM.

    ReplyDelete
  3. Hahaha nchi inavituko hii dhaa

    ReplyDelete
  4. zamani zilikuwa zinaliwa na wala husikii kurudisha kweli KASI YA MAGU NI NOMA

    ReplyDelete
  5. Hii inaonesha Mwanko mpya Chini ya Baba JPJM. Leo pesa zimebaki na zimerudishwa Miaka ile zingewekewa hoja HEWA na zingepeperushwa bila ya kujulikana... Hii inaonesha Uaminifu unaanza kurudi na Ubadhirifu unaanza kuchukiwa kama Awamu yetu ya TANo inavyo kwenda na Huu ndiyo mwendo sahihi japo kuwa wameomba Jengo na Mtukufu Raisi amekubali na amependekeza liwe DODOMA..Sisi pia tunashukuru pia litajenga na kuchangia Ajiri kwa Wadodo wa kukaya wenye uchungu na Ajira na Maendeleo... MULUNGU YAKUTAZE JPJM... Na sisi tunasema Hatuto kuangusha MKULU ... Sandenyi Woooseeeee... JPJM hapa KAZI TUUU

    ReplyDelete

Top Post Ad

Below Post Ad