Kuolewa sio bahati, USIBAHATISHE


“KUOLEWA NI BAHATI!!” hii kauli ina ukweli kiasi gani kwako?! Unaamini kuolewa ni bahati??
Kuna wanaume na wanawake ambao wanaamini  kwamba mwanamke anapoolewa tu basi amebahatika sana bila ya kujali kaolewa na mtu wa aina gani na kwasababu zipi. Ambapo ni sawa na kusema kwa kuolewa, mwanamke anakua amefanyiwaFAVOUR, AMESAIDIWA au AMEPEWA ZAWADI kwa kuolewa kana kwamba mwanamke pekee ndie anaefaidika na ndoa. Na hiyo bahati yenyewe inayotokana na kuolewa huko sio kupata mume ambae anastahili kuitwa mume bali ni kupata mahali pa kulala, chakula na mavazi. Wengine hua wanafika mbali kiasi cha kuwauliza wenzi wao  moja kwa moja “unalalamika nini wakati unakula, unalala na unavaa vizuri?” 

pale mwanamke anapoonyesha kutoridhisha na namna mahusiano yao ndani ndoa yanavyoenda mf. mume kutokua mwaminifu,  kutokuwepo nyumbani muda wa kutosha,  kulewa sana, kumdharau mkewe n.k .

Je, ina maana wanawake wanaolewa ili wale, walale na wavae? Walipokua kwa wazazi wao au wakijitegemea waliishi bila kula, kuvaa na kulala ndani ya nyumba?
Kinachosikitisha zaidi ni kuwa baadhi ya wanawake wanaunga  mkono mawazo haya. Wanakubali kuchukuliwa kama watu wanaopewa msaada kwa kuolewa.

Ladies, wahenga waliposema “Majuto ni mjukuu.” hawakukosea hata kidogo. Siku zote majuto huja baadae. Usikimbilie ndoa kwa minajili ya kukamatia‘BAHATI’ chini alafu baadae ukashangaa wewe ndo umekamatiwa chini na ndoa ambayo kila ukilala, kila ukiamka unajiuliza ilikuwaje ukakubali kuolewa na uliyeolewa nae. Usishinikizwe na mtu ama jambo lolote lile kuingia ndoani bila kuwa na uhakika huyo unaeingia nae ndio mtu sahihi kwako. Tumia muda wa kutosha kufanya tathmini kabla ya kufanya maamuzi.
Kuna mambo kadhaa ambayo naamini yanaweza kusaidia sana katika kufanya tathmini…
Mnapokuwa mmetofautiana/mmegombana huwa unajuta kumfahamu ama kuwa kwenye mahusiano nae?Jiulize, utakuwa wapi miaka 5 ijayo? Unajiona ukiwa na unayetarajia kuolewa nae?Mvue / mnyang’anye mtarajiwa wako mali na cheo alichonacho alafu uangalie je, bado unajiona ukiolewa nae? Yani kesho na kesho kutwa mwenzio kibarua kimeota nyasi, hela hana utamkimbia au utaendelea kuwa nae na kum-support?Mungu aepushie mbali mtarajiwa wako amepata ajali na kupoteza kiuongo cha mwili wake/mwili wake unaacha kufanya kazi vizuri ama anapata ugonjwa ambao unamuondolea uwezo wa kujitegemea na kujihudumia hata kwa mambo madogo madogo tu, UTABAKI NAE?Na je, ikitokea kwamba wewe ndio umepatwa na matatizo (umefulia, huna kazi, mgonjwa hujiwezi, umepata ukilema n.k) UNAAMINI kwamba mtarajiwa wako atakuwa na wewe bega kwa bega bila ya kukudharau na kukusimanga? Maana siku zote majibu yote huwa tunayapata mwanzo kabisa wa mahusiano (mf. mtu ni mbinafsi sana, mnyanyasaji, sio mwaminifun.k) ila huwa tunachagua kupuuza na kukomaa na mahusiano ambayo hayakuwa mazuri tangu mwanzo. (hii mada tutaizungumzia siku nyingine).

BAHATI ya kweli ipo kwenye kumpata mtu ambae anaelewa nini maana ya ndoa na kuiheshimu ndoa yake,  anaempenda mwenzi wake, anaemheshimu mwenzi wake pamoja na mawazo yake,  anaemsikiliza mwenzake,  anaejielewa na kujitahidi kumwelewa mwenzake, aliye tayari kujitoa kwa mwenzake, anaejua na kutimiza majukumu yake, anaejitahidi kumfurahisha mwenzake kwa maneno na matendo. Vivo hivyo kwa wanaume. . . .wenye bahati sio waliooa bali ni waliooa wanawake wenye sifa nilizotanguliza hapo juu. Mtu ambae hata ndani ya moyo wako unajua kabisa ni wako kwa 100% na sio mtu unaeishi nae kwa wasiwasi ama kwa kujilazimisha.
Kuolewa (hata kuoa) sio bahati hivyo usibahatishe.
Tags

Post a Comment

1 Comments
* Please Don't Spam Here. All the Comments are Reviewed by Admin.
  1. Ndoa safi ni mpango wa Mungu. Mimi naishi hapa USA ni meoa mwanamke mzuri mwenye herimu nzuri na pesa nyingi za kutosha, watu wengi na jamaa zangu wanafikilia kwamba ndoa yangu ni nzuri na ni mebahatika kumpata mwanamke mwema kumbe sio hivyo. Natamani sana ningelioa mtu wa kwetu tena masikini ambaye tungelielewana vizuri. Ndoa ya kweli ni ile iliyo barikiwa na Mungu na si vinginevyo!!

    ReplyDelete

Top Post Ad

Below Post Ad