RAIS Jacob Zuma Kutua Nchini na Wafanyabiashara 80..!!!


Rais wa Afrika Kusini, Jacob Zuma anatarajiwa kufanya ziara ya siku tatu nchini kuanzia Mei 10 - 12, mwaka huu akiwa ameambatana na mawaziri sita na zaidi ya wafanyabiashara 80.

Katika ziara hiyo, Rais Zuma atakuwa na mazungumzo na mwenyeji wake, Rais John Magufuli na baadaye kufanya mazungumzo ya pamoja kati ya ujumbe wa Afrika Kusini na ujumbe wa Tanzania.

Akizungumzia ziara hiyo leo, Waziri wa Mambo ya Nje, Dk Augustino Mahiga amesema Serikali za Tanzania na Afrika Kusini zitatiliana saini zaidi ya mikataba 10 kwenye sekta za biashara, uwekezaji, miundombinu, utalii, elimu, afya na nishati.

"Kwa kuanzia tutatiliana saini mkataba wa utunzaji wa mazingira (biodiversity), uchukuzi na nishati. Hiyo mingine bado inaandaliwa, itasainiwa baadaye," amesema Dk Mahiga.

Waziri huyo amesema nchi za Afrika Kusini na Tanzania zimeamua kutumia uhusiano wa kihistoria kama fursa ya kuanzisha uhusiano mpya wa kiuchumi kwa kuongeza uwekezaji na biashara.

Amesema uwekezaji wa Afrika Kusini hapa nchini umezidi kuongezeka kutoka Dola za Marekani 803 milioni mpaka kufikia Dola bilioni 2.2 mwaka 2016 na kuifanya nchi hiyo kuwa ya pili kwa kuwa na uwekezaji mkubwa nchini baada ya Uingereza.

"Uwekezaji wa Watanzania nchini Afrika Kusini bado ni duni, zipo fursa nyingi kule lakini hazijatumika vizuri. Hii ni nafasi kwa wafanyabiashara wetu kuzungumza na wenzao wa Afrika Kusini," amesema.

Katika ziara hiyo, Zuma atashiriki mkutano wa wafanyabiashara, atazindua jengo la Ubalozi wa Afrika Kusini na kutembelea Taasisi ya Moyo ya Jakaya Kikwete.
Tags

Post a Comment

0 Comments
* Please Don't Spam Here. All the Comments are Reviewed by Admin.

Top Post Ad

Below Post Ad