Zitto Kabwe Arusha Dongo Gizani....Je Amemlenga Nani Katika Huu Ujumbe Wake?


Madikteta huchukia mawazo mbadala na sio kelele. Hivyo, Madiketa wengi huondolewa madarakani sio kwa nguvu ya umma ( popular uprising ) bali Kwa mapinduzi ya ndani ( internal coups ) Ili mtawala mwenye sifa za kidikteta aweze kuhimili na kustahmili mikiki ya siasa na kubakia kwenye utawala, anapaswa kufanya moja Kati ya yafuatayo;


- atatii matakwa na matamanio ya Chama alichotumia kuingia madarakani Kwa ukweli kwamba wanaweza kumwajibisha Kwa kumwondoa madarakani kwa sababu anatekeleza sera ambazo wenye chama hawapendi. Ama; 


- Atatafuta njia za kuwadhibiti wenye Chama Kwa kuwapunguzia nguvu ndani ya Chama Mtawala dikteta akiamua kufuata njia ya kwanza Kwa vyovyote vile hatakuwa salama ( insecure ) kwenye utawala na atajikuta ni ' puppet' wa wenye chama.


Akifuata njia ya pili, wenye Chama watajaribu kumzuia Kwa sababu maisha Yao ya kisiasa yatakuwa hatarini ama hata maisha yao binafsi kuwa hatarini. Ndio maana miaka ya mwanzo ya watawala huwa ni miaka yenye migongano ya kugombania madaraka ( power struggles ) huku wenye chama wakijaribu kuhakikisha kuwa mtawala anaondoka mapema zaidi madarakani. Tafiti zinaonyesha kuwa Hali hiyo inaweza kuleteleza mambo matatu makubwa Kwa ujumla


- Mtawala Dikteta atawaburuza wenye Chama; ama 

- Mtawala dikteta atawaweka karibu wenye chama; ama 

- Mtawala dikteta ataanzisha Chama kingine au ataanzisha kundi lake ndani ya Chama Kwa kuwagawa wenye Chama na hivyo kuwa ngumu kuweza kuchukua maamuzi ya pamoja.


Hakuna dhamana ( guarantees ) kwamba mtawala dikteta ataweza kupatia Kwa kuchagua mkakati sahihi kwenye mazingira ya Nchi husika. Akikosea chaguo katika mikakati lazima atapinduliwa au kuondolewa madarakani.


Hata hivyo tafiti zinaonyesha kwamba kuna nchi ambazo watawala madikteta huweza kukaa madarakani muda mrefu Sana kwa sababu huweza kuchagua mkakati sahihi. Vile vile kwenye nchi ambazo mali za watu zinanyanganywa na tabaka tawala kupoteza mali Zao na matumaini ya maisha ya mbele, mtawala dikteta huondolewa mapema zaidi. Mwenendo wa uchumi na kipato cha wananchi ni kiashiria kikubwa Sana cha kudumu au kutodumu kwa mtawala dikteta.


Historia inaonyesha kuwa Madikteta duniani huchukia zaidi wapinzani wenye mawazo mbadala na kudharau wapiga kelele. Madikteta huogopa mawazo na si kelele. Ni harakati za wenye mawazo mbadala Ndio huweza kuleta mabadiliko na harakati za wapiga kelele husindikiza mabadiliko. Muhimu Kwa wenye mawazo ni kuhimili misukosuko na kuruka viunzi.


Zitto Kabwe 

Kibingo, Mwandiga, Kigoma 

Machi, 2017


NB: Maneno hayo ni kutoka kwenye ukurasa wa kiongozi huyo wa Facebook

Post a Comment

1 Comments
* Please Don't Spam Here. All the Comments are Reviewed by Admin.
  1. Mbona mnachagua coment za kuweka. Tunaandika hamziweki hadharani mnabaki sema hamna coments. Vipi? Kazi tu au?

    ReplyDelete

Top Post Ad

Below Post Ad