KIMENUKA...Wafuasi 51 wa Chadema Wakamatwa na Polisi, Chato

Wafuasi na Viongozi  51 wa Chama Cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema) waliokamatwa jana Ijumaa  wakiwa kwenye kikao cha ndani wilayani Chato wanaendelea kushikiliwa na polisi kwa mahojiano.

Miongoni mwa waliotiwa mbaroni wanaoendelea kusota mahabusu ni pamoja na Mwenyekiti wa Chadema Mkoa wa Geita, Fabian Mahenge na Katibu wake, Sudi Kanganyala.

Mwenyekiti wa Serikali kijiji cha Mkuyuni, Anaclet Twegosora, ambaye pia ni Mwenyekiti wa chama hicho Kata ya Chato, amewataja viongozi wengine wanaoshikiliwa kuwa ni mwenyekiti wa Baraza la Wazee mkoani Geita, Vitus Makange na Neema Chozaire ambaye ni Mwenyekiti wa Bavicha mkoa.

Wengine ni Kaimu Mwenyekiti wa Chadema Wilaya ya Chato, Uhuru Selemani, Katibu wake Mangesai Rudonya na diwani mstaafu kata ya Muganza, Marko Maduka.

Kama ilivyokuwa jana, hakuna kiongozi wa Jeshi la Polisi anayekuwa tayari kulizungumzia suala hili.

Wakati Mkuu wa Polisi Wilaya ya Chato, Alex Mkama, ambaye tukio hilo linaendelea wilayani kwake akisema hawezi kulizungumzia, Kamanda wa Polisi Mkoa wa Geita, Mponjoli Mwabulambo, amesema yuko likizo na kuelekeza atafutwe kaimu wake Allan Bukumbi ambaye tangu jana hapokei simu yake ya kiganjani wala kujibu ujumbe mfupi wa maneno anaotumiwa.

Makamu Mwenyekiti wa Chadema Kanda ya Ziwa Victoria, Ansbert Ngurumo, amesema kutawanywa kwa mabomu ya machozi na kukamatwa kwa viongozi na wanachama hao ambao walikuwa katika mkutano wa ndani ni kinyume cha sheria kwa sababu vikao vya ndani havihitaji kutoa taarifa wala kibali cha polisi kwa mujibu wa sheria namba 5 ya vyama vya siasa ya mwaka 1995.
Tags

Post a Comment

1 Comments
* Please Don't Spam Here. All the Comments are Reviewed by Admin.
  1. Inasikitisha sana unyanyasaji wa Watanzania wasio na hatia. Hii inaleta picha mbaya. Sisi wote Watanzania tunalilia maendeleo. Kisa ni nini? Sasa tutaiendelezaje nchi kwa hili kama viongozi kufanya kazi ni dhambi? Sielewi. Mwmenye jibu labda anifundishe.

    ReplyDelete

Top Post Ad

Below Post Ad