Maisha Yalivyombadilikia Hawa wa Diamond na Kuanza Kunywa Gongo

Hawa wa Diamond anaumwa, amekongoroka na anatia huruma. Mwenyewe hajui anaumwa nini, hajui nini kinachomtafuna lakini mama anajua siri hiyo. Analia usiku na mchana akimuomba Mungu amuokoe mwanaye. Lakini mwenyewe anahisi kuwa huenda ni unywaji wa kupindukia ndiyo adui wa maisha ya mtoto wake.

Hapa inaonesha kuwa kuwa kudhoofu kwa mwili wake kiasi cha wakati mwingine kuvimba miguu kama mama yake anavyosema, kunatokana moja kwa moja na unywaji wa pombe haramu aina ya gongo.

Hawa ni msanii aliyeibuliwa na msanii wa Bongofleva, Nassib Abdul (Diamond Platnumz) kwenye moja ya singo zake za mwanzo kabisa ‘Nitarejea’ iliyotoka mwaka 2014. Ikumbukwe kwamba licha ya Diamond kumshirikisha katika wimbo huo, walikuwa wapenzi kiasi ambacho Diamond alikuwa hatoki nyumbani kwa hawa.

Ukiangalia video ya wimbo huo na ukamuangalia vizuri, basi ujue si hawa huyu wa sasa kwa sababu unaweza kutokwa machozi. Achilia mbali kukanda, lakini urembo aliokuwa nao umekwisha kiasi hata mama yake mzazi anaonekana kijana kuliko yeye.

Hawa na mama yake kwenye kipindi kimoja cha televisheni nchini walikuwa wakielekea ni nini kilichomsababishia kuwa hivyo na ni vipi ataondokana na hali hiyo ili kuendeleza kipaji chake alichopewa na Mwenyezi Mungu, cha kuimba.

“Ni makundi tu ndiyo yaliyoniponza. Nilikuwa nakunywa pombe ya aina yoyote ile, hata gongo, ilimradi tu nilewe, nibembee,” amesema Hawa. Baada ya wimbo huo alioshirikishwa na Diamond, alitoa ngoma yake mwaka 2015 aliyoiita ‘Mawazo’ amabapo amesema kuwa kitu kingine kilichomfanya kuingia kwenye kadhia ya unywaji ni mawazo kama jina la wimbo wake baada ya mzazi mwenzake kumtelekeza na mtoto, lakini pia mzazi mwenzake huyo ndiyo chanzo cha yeye kunywa pombe, kwani alimfundisha kwa kumnunulia bia.

“Aliponiacha nilikuwa nimeshazoea kunywa. Mawazo ya kutelekezwa yalinifanya nitake kuendelea na unywaji zaidi, lakini uwezo sina, kwahiyo nikajikuta nakunywa kila aina ya pombe ya kienyeji ya bei nafuu inayopatikana,” alibainisha.

Mama mzazi wa msanii huyo mara kwa mara mazungumzo yake yalikuwa yakikatishwa na kilio, kilio cha uchungu kama mzazi. Kwanza alikiri kuwa binti yake ni mnywaji zaidi wa pombe ya kienyeji aina ya gongo. Pia alisema kuwa hata mtoto anayedai Hawa kuachiwa na mzazi mwenzake ni yeye ndiyo anayemtunza na kumsomesha.

“Mimi ndiyo namtunza huyu mjukuu, mama yake anazurura huko. Mimi natafuta pesa ya ada ndiyo asome, kwa sasa nadaiwa ada,” amesema mama Hawa na kuongeza kuwa miaka mitatu iliyopita binti yake hakuwa hivyo.

“Njiani tukiongozana, yeye ndio anapata ‘shikamoo’ na mimi naonekana kijana,” ameongeza.

Hawa amesema kuwa anataka kubadilika na kwa kuanza ameamua kuacha pombe za aina zote. Pia amewaomba wasanii Diamond Platnumz, Barnaba na Nay wa Mitego wamsaidie ili aweze kushaini tena.
Tags

Post a Comment

0 Comments
* Please Don't Spam Here. All the Comments are Reviewed by Admin.

Top Post Ad

Below Post Ad