Kofi Annan Amshauri Odinga Kufuata Njia Sahihi za Kisheria


Kofi Annan Amshauri Odinga Kufuata Njia Sahihi za Kisheria
Kofi Annan alikuwa mpatanishi mkuu mzozo wa baada ya uchaguzi Kenya mwaka 2007
Katibu mkuu wa zamani wa Umoja wa Mataifa Kofi Annan, ambaye alikuwa mpatanishi mkuu baada ya mzozo wa kisiasa nchini Kenya miaka kumi iliyopita, ametoa wito kwa walioshindwa kutumia mifumo ya kisheria kutafuta haki.

Bw Annan alikuwa mpatanishi mkuu baada ya ghasia kuzuka baada ya uchaguzi mkuu wa 2007 uliokumbwa na utata.

Bw Mwai Kibaki alitangazwa mshindi wakati huo lakini Bw Raila Odinga na chama chake cha ODM wakapinga matokeo hayo.
Katibu mkuu huyo wa zama ni wa UN amempongeza Bw Kenyatta kwa ushindi wake na pia akamsifu Bw Odinga kwa kuendesha kampeni yake kwa njia ya amani.

"Namshukuru kiongozi wa upinzani Raila Odinga kwa kampeni ya uchaguzi ya amani aliyoiendesha. Amekuwa mtetezi jasiri wa demokrasia," amesema Dkt Annan kupitia taarifa.
"Kwa hivyo, namhimiza sasa afuatilie malalamiko yake kupitia mifumo ya kisheria iliyowekwa na aweke maslahi ya taifa mbele, kama alivyofanya kwa uzalendo mara nyingi awali."
Upinzani umekuwa ukidai mitambo ya Tume ya Taifa ya Uchaguzi (IEBC) ilidukuliwa na matokeo kuchakachuliwa kumfaa Rais Kenyatta.

Bw Annan pia ametoa wito kwa Rais Kenyatta, ambaye alitangazwa mshindi wa urais Ijumaa afanye juhudi kuunganisha tena taifa.

Alhamisi, muungano wa upinzani National Super Alliance (NASA) ulidai Bw Odinga ndiye aliyeshinda uchaguzi huo na kuitaka tume hiyo kumtangaza kuwa mshindi.
Rais Kenyatta alipata kura 8, 203, 290 ambayo ni asilimia 54.27 naye mpinzani wake mkuu, mgombea wa muungano wa upinzani wa National Super Alliance Raila Odinga akapata kura milioni 6,762,224 ambayo ni asilimia 44.74.

Maajenti wakuu wa NASA waliondoka ghafla kikao cha tume hiyo cha kuafikiana kuhusu matokeo hayo kabla ya kutangazwa kwa Bw Kenyatta kuwa mshindi wa uchaguzi huo Ijumaa usiku.

Naibu ajenti mkuu wa muungano huo James Orengo, amesema muungano huo hautaenda kortini. Amesema hawana imani na idara ya mahakama kwamba itashughulikia malalamiko yao kwa njia ya haki bila mapendeleo.


Kiongozi huyo amesikitishwa na mauaji ambayo yametokea kwenye makabiliano kati ya waandamanaji waliokuwa wanapinga matokeo na polisi.

"Amani, uthabiti na ustawi vinategemea viongozi wa kisiasa Kenya. Wanafaa kuwa makini sana katika mambo wanayosema na vitendo vyao katika hali hii ya sasa. Nawaomba wawajibike."
Naibu rais na mwakilishi mkuu wa Umoja wa Ulaya Federica Mogherini pia ameutaka upinzani kutumia njia za kisheria kufuatilia malalamiko yao kuhusu uchaguzi.

"Sawa na ulivyofanya Umoja wa Afrika, Umoja wa Ulaya unatarajia upinzani uheshimu matokeo na ktuumia njia za kisheria zilizopo kukata rufaa na kuwasilisha malalamiko," amesema kupitia taarifa.
Polisi walikabiliana na wafuasi wa upinzani katika mitaa ya Mathare na Kibera jijini Nairobi, katika katika maeneo ya Homa Bay, Migori na Kisumu ambayo ni ngome ya Bw Odinga magharibi mwa Kenya.

Tags

Post a Comment

0 Comments
* Please Don't Spam Here. All the Comments are Reviewed by Admin.

Top Post Ad

Below Post Ad