Mabasi 18 Yakamatwa kwa Kosa la Kuzidisha Nauli

Mabasi 18 Yakamatwa kwa Kosa la Kuzidisha Nauli
Jumla ya mabasi 18 yamekamatwa kwa siku mbili mkoani Tanga  kwa makosa  ya kuzidisha nauli kwa abiria katika kipindi hiki cha kuelekea sikukuu ya Krismasi na mwaka mpya baada ya Mamlaka ya Udhibiti Usafiri wa nchi Kavu na Majini  (Sumatra)  kwa kushirikiana na jeshi la polisi kuendesha msako maalumu.

Ofisa wa Sumatra mkoa wa Tanga Dk Walukani Luhamba alisema jana kuwa idadi hiyo ya mabasi ilikamatwa kufuatia kufanyika oparesheni iliendeshwa kwa siku mbili kwa lengo la kudhibiti vitendo vinavyofanywa na baadhi ya wenye mabasi kupandisha nauli katika kipindi hiki cha siku kuu za Krismasi na mwaka mpya.

Amesema  mabasi yaliyokamatwa katika oparesheni hiyo  ni yale  yaliyokuwa yakitokea Tanga kuelekea   Dar es salaam , Mbeya, Moshi, Arusha, Dodoma na Morogoro na nchi jirani ya Kenya ambapo mbali ya kuongeza nauli, mengine yalikutwa na makosa ya abiria kutofunga mikanda, mikanda mibovu, na kuzidisha idadi ya abiria kama kulingana na maelekezo ya leseni husika.

“Tumeweka kambi katika barabara kuu eneo la Mkata, Segera, Korogwe na Mombo, hakuna basi litakaloruhusiwa kuendelea na safari, tutawashusha abiria na dereva tutamfikisha mahakamani lakini mmiliki atatozwa faini ya Sh300,000”alisema Dk Walukani.

Ofisa huyo amesema  operesheni hiyo pia itahusisha ukaguzi wa mabasi yanayoondoka jijini Tanga kabla ya saa 12.00 alfajiri kwa sababu ni kinyume cha sheria ya usafirishaji wa abiria.

Hatua hiyo ya Sumatra, imepongezwa na wasafiri waliozungumza na Mwananchi katika kituo kikuu cha mabasi cha Kange Jijini Tanga waliosema kwa kipindi hiki kuna haja ya kuwadhibiti wenye mabasi kwani wanadai ni kipindi chao cha mavuno.

Flora Jonathani  aliyesafiri  kutoka  Dar es salaam hadi Tanga jana  amesema  ameshuhudia  abiria  waliokuwa wakielekea Mkoani Kilimanjaro wakitozwa Sh40,000 kila mmoja ili kuweza kupata nafasi kwenye mabasi.

“Kwenye tiketi wanaandika nauli inayoruhusiwa na Sumatra lakini fedha halisi wanazotoa abiria ni kubwa mno na wanakubali ili waweze kupata usafiri kwenda kwao”amesema Flora.
Tags

Post a Comment

0 Comments
* Please Don't Spam Here. All the Comments are Reviewed by Admin.

Top Post Ad

Below Post Ad