“No uchaguzi, No mabadiliko Yanga”-Mzee Akilimali

Katibu wa baraza la Wazee wa Yanga, m zee Ibrahim Akilimali ameshikilia uzi ulele wa kutaka ufanyike uchaguzi wa kuchagua mwenyekiti wa klabu hiyo kabla ya kuanza mchakato wa mabadiliko ya uendeshaji ndani ya klabu hiyo ya Jangwani.

Mzee Akilimali anaunga hoja ya mabadiliko ya uendeshaji wa klabu hiyo lakini anachotaka ufanyike kwanza uchaguzi wa kumpata mwenyekiti kabla ya kuendelea na mchakato wa mabadiliko.

“Kutaka uchaguzi ndio naonekana napinga maendeleo? Nataka tufanye uchaguzi tuchague mwenyekiti wetu. Wafanye utafiti wanachama wangapi wa Yanga wanataka uchaguzi na wangapi hawataki uchaguzi halafu wapokee maoni na wawe wakweli.”

“Tunatakiwa tufanye uchaguzi tuchague tumpate kiongozi wetu baada ya kumpata kio9ngozi wetu, turudi kwenye katiba yetu maana hili jambo la kampuni lipo kwenye katiba. Ndani ya katiba yetu inaeleza klabu itakuwa na hisa asilimia 51 na wawekezaji watakuwa na asilimia 49, sasa tukishampata mwenyekiti viongozi wetu wanakaa kuandaa mpango wa mabadiliko.”

“Kwenda kwenye mabadiliko huku tukiwa na kaimu mwenyekiti hilo ndio sitaki, na ninajua mbinu hizo zinafanywa na watu wanatayarishwa kwa ajili ya kutuletea vitu vya namna hiyo.kinachofanya tusipate kwanza mwenyekiti ni nini?”

Jana December 18, 2017, viongozi wa umoja wa matawi ya Yanga walitangaza kuwa, wameandika barua kwa kamati ya utendaji ya klabu hiyo wakiomba mzee Akilimali afutwe uanachama wa Yanga kwa madai kwamba wamechoshwa na vitendo vya mzee Akilimali kwenda kinyume na taratibu za klabu hiyo.

Mwenyekiti wa umoja wa matawi ya Yanga Robert Kasela alisema, mzee Akilimali si mwanachama halali wa Yanga hivyo wameona hakuna sababu ya kuendelea kuwa naye kwakuwa siku zote amekuwa akipinga maendeleo ya klabu.

Mzee Akilimali amewajibu viongozi hao wa matawi kwa kusema, kwa sasa wanatakiwa kuangalia ni kwa namna gani wataifunga Mbao kwenye mchezo wao ujao ambapo watakuwa ugenini kwenye uwanja wa CCM Kirumba, Mwanza.

“Tufikirie namna gani tutashindana na Mbao maana mpaka sasa hatujaifunga sisi ndio vitu vya kufikiria wana Yanga sio kufikiria kumuondoa mzee Akilimali, akiondoka Akilimali basi kuna akina Akilimali wengi watakuja na hao kwenye mkutano wataambiwa sio wanachama?”
Tags

Post a Comment

1 Comments
* Please Don't Spam Here. All the Comments are Reviewed by Admin.

Top Post Ad

Below Post Ad