Mo Dewj Aliwapa Sabuni Lakini Akawapaka Matope

Priva ABIUD

Ndugu zangu wa Msimbazi mtanisamehe kidogo. Niwaambieni kitu. Kiki haziumbi kipaji ila zinajenga jina. Nina mawazo tofauti na kauli ya Mo Dewj aliyoitoa akimtaka Omog aondoke. Nafahamu wengi mlikaa kimya.

Wanasema nyumbani kama mdogo wenu ana hela kuwazidi, hamuwezi kufanya lolote kwenye familia bila ridhaa yake. Ni kweli hakuna aliyepinga wala aliyeuliza kwanini Omog ameondoka. Najua wengi mlifyata mkia.

Kaka Mo aliwapa chakula lakini mkiwa mezani mnakula naona aliwatukana. Alisema yeye kama mshabiki wa simba anamuomba Omog anajiuzulu. Najiuliza sababu ni nini? Je Mo akiwa kama shabiki wa simba aliwahi kusimama na ku-post mtandaoni kuwa Omog amekosea nini na ajirekkebishe wapi? Kama ipo hiyo post nijulishwe. Mshindi wa zabuni ya uwekezaji kwenye klabu leo hii anajiita mshabiki, tena isitoshe kwenye mtandao wa kijamii?

Najiuliza, je Mo alikuwa anatafuta kiki? Je ni kweli Mo alishindwa kwenda kwenye bodi na kuwaelezea hisia zake? Hivi ni kweli Mo alikuwa hana uwezo wa kuonana na Omog?

Mbali na hayo hivi Mo anaitambua hadhi yake kwa wana simba? Ina maana Mo anajiona yeye ni sawa na shabiki wa Simba aliyeko Tunduma kwamba ana-post hisia zake anavyojisikia tu? Au tumwite mnafiki? La hasha. Mo sio mnafiki. Sasa tumwiteje?

Niwarudishe nyuma kidogo. Florentino Perez aliongea kauli za kashfa sana mbele ya waandishi wa habari kuhusu kocha wake mkuu. Alimuongelea vibaya sana Del Bosque. Iliichukua Real Madrid zaidi ya miaka 12 kutwaa Ubingwa wa uefa, na kwa kipindi cha miaka minne walibadilishwa makocha sio chini ya watatu. Timu ilishindwa kutulia. Hakuna kitu naheshimu kwa kiongozi kama busara na hekima. Mimi siamini kama Mo anatafuta kiki. Kiki ipi sasa? Yeye tayari bilionea. Au anatafuta atokee kwenye kurasa za magazeti? Hakuna asiyependa kutokea kwenye kurasa lakini je kuna tija?

Roman Abramovic licha ya kuwa bilionea mkubwa, Mourinho aliwahi kupishana nae kwenye vyumba mara kadhaa bila ya kusalimiana. Roman baadae alimfuata Mourinho ana kwa ana akamweleza alichokitaka. Roman hakuwahi ku-post mitandaoni.

Kwanza mimi ningekuwa bosi wa Simba kwa sasa ukurasa wa manara ningeupiga chini. Achague ukurasa wake wa Insta au kazi. Kuna nyadhifa ukiwa nazo hupaswi kuishi kama Soudy Brown wa Shilawadu.

Wewe ni kiongozi mkubwa ukurasa wako unakuwa kama wa Giggy Money? Kisa nini? Ili iweje? Halafu? Ukurasa uliopaswa kutumika kutoa taarifa za simba ni ukarasa wa klabu tu. Wewe ulishawahi kuona Ed Woodward au Jose Mourinho wanapost kwenye kurasa zao kuhusu Chelsea? Au wanaelezea masuala ya ndani ya klabu? Mo utanisamehe kaka. Wewe ni bosi. Sikufundishi ubosi.

Na siamini kama Omog alifukuzwa kwa sababu ya matokeo ya Simba kufungwa na Green Warriors. Najua yalikuwepo mengine. Mngeyamaliza ndani kwa ndani. Jifunzeni soka la kisasa. Nisameheni tu bure.
Tags

Post a Comment

0 Comments
* Please Don't Spam Here. All the Comments are Reviewed by Admin.

Top Post Ad

Below Post Ad