Kombe la EPL sasa nuksi kwa makocha, ukibeba tu msimu ujao unatimuliwa

Mzimu wa kubeba ndoo ya EPL na kutimuliwa umeshaanza kumuandama Antonio Conte, baada ya kuwapa Chelsea taji la EPL msimu uliopita sasa Muitaliano huyo yupo katika hati hati ya kuondoka katika ligi hiyo.

Lakini kwa siku za usoni hii imekuwa desturi ya EPL kwa kocha kuchukua kombe msimu huu na kisha msimu unaofuata anatimuliwa na hii imekuwa kwa makocha karibia wote 6 waliobeba makombe 6 yaliyopita.

Kumbukumbu hii inaanza msimu wa 2011/2012 baada ya Roberto Mancini kuwapa ubingwa Manchester City lakini baada ya ubingwa huo hakudumu, mwaka uliofuata yani 2013 Manchester City wakamtimua na nafasi yake kwenda kwa Manuel Pellegrini.

Baada ya Manchester City kuchukua ubingwa wa 2011/2012 msimu uliofuata wakawapa kombe Manchester United waliokuwa chini ya Alex Ferguson lakini kwa SAF hakuondoka bali msimu ulipoisha tu alistaafu.

2013/2014 Manchester City tena chini ya Manuel Pellegrini walichukua kikombe cha EPL lakini kabla hata ya msimu haujaisha Pellegrini alitangaza kwamba ataachana na City itakapofika mwaka 2016.

Jose Mourinho naye msimu wa mwaka 2014/2015 akabeba kombe la EPL, mwaka huo huo 2015 ambao Mourinho alichukua ubingwa mwezi wa 12 Chelsea waliamua kumfungashia virago na moja ya sababu ikiwa ni kutokuelewana na wachezaji pamoja na ugomvi na daktari Eva Carneiro.

Ilipofika msimu wa 2015/2016 Claudio Ranieri akafanya kile ambacho wengi hawakukitaraji baada ya kuwapa Leicester ubingwa wa EPL na mwaka 2017 dunia ikaamini hakuna huruma tena katika soka baada ya Leicester kumuonesha Ranieri mlango wa kutokea.

2016/2017 ndio msimu uliopita na ni zamu ya Antonio Conte sasa, kwa hali ya mvutano na kiwango cha Chelsea haihitaji akili kubwa kujua ni nini Roman Abromovich atakachomfanya hivi karibuni.
Tags

Post a Comment

0 Comments
* Please Don't Spam Here. All the Comments are Reviewed by Admin.

Top Post Ad

Below Post Ad