Watanzania Nani Katuroga?

Na Priva Abiud

Kwenye mechi ya Yanga wengi waliamini tumeenda kuhani msiba ila mechi ya Simba wengine wakaamini ndio siku ya mazishi yenyewe. Sitaki kuongelea sana ubora wa mechi yenyewe ila namna tulivyojiandaa. Kimsingi kulikuwa na idadi ndogo sana ya mashabiki uwanjani hasa hasa mechi ya Yanga. Hata Robo ya uwanja haikufika.

Wakati wa mahojiano nilipata bahati ya kuongea na kocha wa Township Rollers pia nilipata bahati ya kipekee kumhoji kocha mkuu wa Al Masry. Wote nilijaribu kujua mapokezi ya watanzania wameyaonaje.

Lengo langu ni kuwachokonoa kuwa wamejisikiaje tokea wanafika uwanja wa ndege mpaka uwanjani. Kocha wa Rollers alisema (All Tanzanians are beautiful, am truly satisfied) (amewapongeza watanzania na ameridhika). Kocha wa Al Masry akanijibu akaniambia (your amazing, we shall respect you) (watanzania mmetisha, na tutawaheshimu). Kocha wa Al Masry tena alinigeukia kabisa, nina imani alitabiri kuhusu swali langu na alifahamu vyema nimeliuliza kwa makusudi. Alifahamu wazi kuwa alichokutana nacho ni cha ajabu, mwarabu kushangiliwa na mtu mweusi tena kwenye ardhi ya watu weusi.

Amegundua ‘uzwazwa’ wetu hapa nchini. Amefahamu hatuna mshikamano hata kidogo. Waarabu na sisi ni ngozi tofauti kabisa. Amegundua kuwa kisaikolojia hawa hakuna kitu. Siwalaumu Simba wala siwalaumu Yanga ila nawalauamu watanzania. Haiwezekani kila mwaka timu ya taifa haifanyi vizuri halafu makelele tunayatupia TFF na kwa wachezaji.

Moja ya mambo ambayo Gomaa, Koffi na Ahmed waliyofurahishwa nayo sio matokeo ya magoli mawili ya ugenini, ni kwa namna tulivyowapokea na kuwashangilia utadhani sisi ni koloni la Hussein Mubarak. Mbaya zaidi kuna kijana mmoja aliomba jezi ya Ahmed jamaa akamwambiaa noooo (halafu na maneno ya kiarabu, mimi nahisi yale yalikuwa matusi) unadhani Simba wakienda Misri watatuchukuliaje? Je na nyie Yanga mkienda Misri Zamalek watawashangilia? Simba je? Mnadhani mkienda Botswana BDF watawapa shavu? Huko timu zenu zinakoenda nani atazishangilia? Kwa nini usibaki nyumbani kama timu yako haichezi?

Leo hii Simba atafungwa na waarabu, kesho Yanga mkienda si watajua ni wale wale wenye chuki za wenyewe kwa wenyewe. Wakija hapa wanajua wazi tuna mashabiki. Sio kwamba hawazijui Simba na Yanga wanazifahamu vyema na wanafahamu uendawazimu wetu ni utani wa jadi. Labda nikwambie kitu. Wakati mchezo haujaanza nilifika uwanjani saa 9. Upande wa kulia mwa uwanja palikiwepo mashabiki kama 50 hivi wa Yanga. Mwandishi mmoja wa CN Sport ya Misri akaenda makusudi kabisa kwenye lile jukwaa kuwapiga picha mashabiki wa Yanga waliokuwa wanamshangilia. Mashabiki wa Yanga wakafurahi na kuongeza spidi kweli… hivi kule CN Sport wakiwaoan hao waarabu si wanatuona kama watumwa wao? Hivi ni picha gani tumejenga kwa wabotswana na wa Misri?

Shida ipo wapi? Ni mpira gani huu? Soka letu litakuwa endapo tu pale timu mbalimbali zikija hapa zikala kichapo cha haja. Kinachokuza ligi zetu za ndani ni ushirikiano tu. Leo kocha wa Township Rollers anasema nilikuwa naijua hii mechi kabla ya hapo. Wala sikujishughulisha sana. Ivan Ntege anasema walijua timu za Tanzania ni dhaifu mno.
Kwa mfano tu, tukienda nje ya nchi yetu viwanja vyao vinakaribia kujaa. Vilabu husika vifanye yafuatayo. Kwa mfano kama tiketi ni 5000 nunueni tiketi 20,000 uzeni kwa bei ya shilingi 3000 jazeni mashabiki uwanjani kwenye mechi muhimu kama hizi. Mpira ni mashabiki. Umeona namna Simba walivyoshangilia kwa ari kubwa uwanjan? Licha ya kwamba walikuwa nusu, hivyo hivyo Yanga nao wanapaswa kufanya. Jazeni uwanja. Shangilieni kila dakika. Morali ndio kila kitu. Simba ikitoka haimfaidishi chochote Yanga, wala Yanga wakitoka haisaidii chochote.

Lakini moja wao anapofanikiwa ndiko wachezaji wetu wanasonga mbali wanaonekana na wanaenda vilabu vikubwa. Hakuna mchezaji anayefanikiwa kwa kushiriki kombe la Mapinduzi chuki zetu zibaki ndani taifa kwanza. Njia pekee michuano ya kimataifa.

Tunaendaje kule kama tutapigana vikumbo? Kazi ya matawi ya hizi timu ni nini? Kujazana ujinga? Mzee ana miaka 50 unaenda washabikia wageni? Ushauri wangu tu, Simba na Yanga jazeni mashabiki uwanjani. Wekeni tiketi kwa bei nafuu kila mtu aende taifa. Nchi za wenzetu wakati fulani watu wanajaa uwanjani bureee ili tu wasapoti timu zao. Leo jitu zima linatoa 10,000 kwenda kushabikia timu za nje? Ni undondocha huo.
Tags

Post a Comment

1 Comments
* Please Don't Spam Here. All the Comments are Reviewed by Admin.
  1. Acha hayo mambo ya Mpira wanaakili za hovyo na kama utumwa dhahiri utaruhusiwa rasmi tena duniani watanzania watakuwa wakwanza kutawaliwa.

    ReplyDelete

Top Post Ad

Below Post Ad