Waziri Matiang'i: Miguna Lazima Aombe Tena Uraia wa Kenya ili Aruhusiwe Kuingia Kama Raia

Waziri Matiang'i: Miguna Lazima Aombe Tena Uraia wa Kenya ili Aruhusiwe Kuingia Kama Raia
Waziri wa mambo ya ndani nchini Kenya Dkt Fred Matiang'i amesema mwanasiasa wa upinzani aliyetimuliwa nchini humo Miguna Miguna atalazimika kuomba tena uraia.

Waziri huyo amesema Bw Miguna alipoteza uraia wake alipouchukua uraia wa Canada mwaka 1988 na hawezi kuruhusiwa kuingia nchini Kenya kama raia bila kuomba tena uraia.

Dkt Matiang'i, aliyekuwa akihojiwa na kamati ya bunge, amesema mwanasiasa huyo ambaye pia ni wakili alijipatia paspoti yake ya Kenya na kitambulisho cha taifa anachokitumia kwa sasa kwa njia ya ulaghai.

Waziri huyo amesema hakuna shaka kwamba Bw Miguna alizaliwa Kenya.

"Yeyote aliyechukua uraia wa taifa jingine kabla ya katiba ya sasa kuidhinishwa mwaka 2010 ambaye anafikiri kwamba ataweza kurejea bila kufuata utaratibu uliowekwa anajihadaa.

"Hapana shaka kwamba Miguna alizaliwa Kenya. Lakini kwa mujibu wa katiba ya kabla ya 2010, yeyote aliyechukua uraia wa nchi nyingine alipoteza uraia wake wa Kenya. Bunge liliidhinisha sheria inayoeleza jinsi mtu kama huyo anavyoweza kuupata tena uraia wake."

Waziri huyo pia amejitetea dhidi ya shutuma kwamba amekuwa akikaidi maagizo ya mahakama ya kutaka Bw Miguna aachiliwe huru na kuruhusiwa kuingia Kenya.

Jaji wa Mahakama Kuu George Odunga alikuwa ameagiza Dkt Matiang'i, pamoja na mkuu wa polisi Joseph Boinnet, mkuu wa idara ya uhamiaji Gordon Kihalangwa na katibu wa wizara ya mambo ya ndani Karanja Kibicho wafike mbele yake kueleza ni kwa nini walikosa kutekeleza amri ya mahakama ya kumruhusu Bw Miguna aingie Kenya.

Miguna asafirishwa kutoka Dubai kwenda Canada
Dkt Matiang'i amesema: "Jaji alipokuwa anatutaka tufike mbele yake tulikuwa tunahudhuria sherehe za kufuzu kwa maafisa wa polisi wa kukabiliana na fujo (GSU). Tulihukumiwa bila kupewa fursa ya kujieleza, kwa kutumia madai ya uongo."

Jaji Odunga aliwapiga faini maafisa hao Sh200,00 kila mmoja, na akaagiza pesa hizo zikatwe kutoka kwa mishahara yao.

Dkt Matiang'i pia amepuuzilia mbali madai kwamba serikali ilimfurusha Bw Miguna kutoka nchini humo akisema hatua kama hiyo ingehitaji idhini yake.

Bw MigunaHaki miliki ya pichaAFP/GETTY
Image caption
Miguna aliwasili uwanja wa JKIA Jumatatu wiki iliyopita lakini akazuiwa kuingia nchini Kenya
"Hakufurushwa kutoka Kenya. Nilihitaji kutia saini idhini ya kumfurusha. Hatungemfurusha kwani hakuwa ameingia bado ndani ya eneo la utawala wetu," Dkt Matiang'i amesema.

"Tulimuondoa uwanja wa ndege kama mtu ambaye hakuwa na stakabadhi za kumtambua, abiria ambaye hangetambuliwa ambaye kawaida hurejeshwa alikotoka."

Waziri huyo amesema Miguna hataruhusiwa kurejea Kenya bila kuomba kurejeshewa uraia wa Kenya.

Katiba ya kabla ya 2010 haikuruhusu uraia wa nchi mbili kama ilivyo kwa katiba ya sasa.
Tags

Post a Comment

0 Comments
* Please Don't Spam Here. All the Comments are Reviewed by Admin.

Top Post Ad

Below Post Ad