Ofisa Mauzo Kizimbani Kwa Kuchapisha Taarifa za Uchochezi Telegram

Ofisa Mauzo wa Kampuni ya Aggrey&Clifford, Razack Hamad (26) amefikishwa Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu akikabiliwa na kosa la kuchapisha taarifa za uchochezi kupitia mtandao wake wa Telegram.

Wakili wa serikali, Patrick Mwita amedai mbele ya Hakimu Mkazi, Martha Mpazi kuwa mshtakiwa anakabiliwa na kosa la kuchapisha taarifa ya uchochezi kinyume na kifungu cha 53(1)(c) na 52(1)(a) cha Sheria ya Habari Namba 12, ya mwaka 2016.

Inadaiwa mshtakiwa ametenda kosa hilo, Machi 9, mwaka huu akiwa jijini Dar es Salaam ambapo alitumia mfumo wa kompyuta katika simu yake kupitia mtandao wake wa Telegram kwa kuandika; “Nimepata wazo kwa group jingine huko tunaweza kukwepa gharama pia kuandika hata kwenye kuta za wazi #April 26 Magufuli Out, Pinga Dictator” Maneno ambayo yangeibua chuki kwa Watanzania.

Mshtakiwa amerudishwa rumande kwa kushindwa kutimiza masharti yaliyomtaka kuwa na wadhamini wawili watakaosani bondi ya Sh milioni tano. Kesi hiyo imeahirishwa hadi Mei 24, mwaka huu.
Tags

Top Post Ad

Below Post Ad