Ufaransa Yaishutumu Marekani kwa Kuiwekea Vikwazo vya Biashara Iran

 Ufaransa Yaishutumu Marekani kwa Kuiwekea Vikwazo vya Biashara Iran
Ufaransa imesema kuwa haitokubali hatua ya Marekani kuziwekea vikwazo kampuni zinazofanya biashara na Iran.

Kitendo hicho cha Washington kinajiri kufuatia hatua ya rais Donald Trump kujiondoa katika makubaliano ya kihistoria ya kusitisha mpango wa kinyuklia wa Iran.

Waziri wa maswala ya kigeni nchini Ufaransa Jean-Yves Le Drian alisema kuwa kampuni za Ulaya hazifai kuathirika kutokana na uamuzi wa Marekani.

Marekani inasema kuwa kampuni zina miezi sita kusitisha biashara na hazitaruhusiwa kuandikisha kandarasi mpya la sivyo zikabiliwe na vikwazo.

Katika mahojiano na gazeti la Le Perisien waziri huyo wa maswala ya kigeni alisema: Tunahisi kwamba hatua ya kupita mipaka ya vikwazo hivyo haitakubalika. Raia wa Ulaya hawafai kuathirika na hatua ya Marekani kujiondoa katika makubaliano ambayo wao wenyewe walishiriki.
Tags

Top Post Ad

Below Post Ad