Wakili Alalamika Mke wa Seth Kukataliwa Kumuona Mumewe Mahabusu

Wakili  Alalamika Mke wa  Seth Kukataliwa Kumuona Mumewe Mahabusu
Wakili wa Harbinder Seth, Dora Mallaba amelalamika kuwa, mke wa mteja wake, amezuiwa kumuona mume wake mahabusu.

Akizungumza leo Mei 10, mbele ya  Hakimu Mkazi wa Mahakama ya Kisutu, Huruma Shahidi, Wakili  Mallaba amesema kibali cha mke wa Seth kumuona mume wake gerezani kiliombwa tangu Februari mwaka huu lakini hadi leo hakijatoka.

 Ameiomba Mahakama  kutoa maelekezo ili mke wa Seth, akamuone mume wake gerezani.

Pia wakili huyo, amelalamika kuwa Sethi alipelekwa hospitali ili apimwe na kupewa majibu ya vipimo kutokana na hali yake ya kiafya kuwa mbaya, lakini hajapewa majibu hayo mpaka sasa.

Baada ya Dora kueleza hayo, Shaidi alidai kuwa amri ya Mahakama imetekelezwa kwa kumpeleka Seth hospitali na kwamba suala la matibabu halipaswi kuingiliwa na mahakama liachwe baina ya mgonjwa na madaktari.

Kuhusu mke wa Seth kuzuiwa kumuona mumewe, Shaidi amedai kuwa sheria ya magereza ipo wazi na kwamba imetoa utaratibu wa kumuona mtu aliyekuwapo mahabusu.

Soma Zaidi: Hakimu akerwa bilionea IPTL kutopatiwa matibabu Muhimbili

“Ni rai yetu wafuate utaratibu za Magereza walizoelekezwa ili mke apate nafasi ya kumuona mumewe," ameeleza Shaidi.

Baada ya kusikilizwa hoja hizo, Hakimu Shaidi amesema suala la kuonana na mtu aliyekuwepo magereza ni la kibinadamu kwani hao ni mtu na mkewe na wanapendana hivyo alishauri wapewe nafasi ya kuonana.

Hakimu Shahidi ameiahirisha kesi hadi Mei 25, 2018 kwa ajili ya kutajwa.

Seth ni mmiliki wa Kampuni ya Kufua Umeme ya Independe Power Tanzania Ltd(IPTL) na James Rugemarila, Mmiliki wa kampuni ya VIP Engineering and Marketing.

 Wanakabiliwa na mashtaka  12 ya  uhujumu uchumi  kwa kula njama, kujihusisha na mtandao wa uhalifu , kughushi,  kutoa nyaraka za kughushi, kujipatia fedha kwa njia za udanganyifu,  kutakatisha fedha  na kuisababisha serikali hasara .

Tags

Top Post Ad

Below Post Ad