China Yaiomba Tanzania Kuwa Mwenyeji Wa Mkutano Wa Kidunia Wa Viongozi Wa Vyama Vya Siasa



Chama Cha Mapinduzi (CCM) kimeombwa kuwa mwenyeji wa Mkutano wa kidunia wa viongozi wa vyama vya kisiasa, maombi haya yamewasilishwa na Balozi wa China nchini Tanzania Bi. Wang Ke alipotembelea Ofisi Ndogo ya Makao Makuu ya CCM Lumumba kuonana na Ndg. Bashiru Ally Kakurwa, Katibu Mkuu wa Chama Cha Mapinduzi (CCM).

Katika salamu zake Balozi Wang Ke ameeleza China na Chama Cha Kikomunisti cha China (CPC) kinampongeza Ndg. Bashiru na kwamba wako tayari kushirikiana naye katika masuala mbalimbali kama sehemu ya mahusiano ya muda mrefu kati ya Tanzania na China na vyama vya CCM na CPC.

Aidha, Balozi Wang ametumia mkutano huo kuwasilisha ombi la China kwa Chama Cha Mapinduzi kuwa mwenyeji wa Mkutano wa Kidunia wa Viongozi wa Vyama vya Siasa ambao kwa mara ya kwanza unafanyika barani Afrika na unaotarajiwa kufanyika mwezi wa Julai 2018.

Chama Cha Kikomunisti cha China (CPC) kimeichagua Tanzania na Chama Cha Mapinduzi (CCM) kuwa mwenyeji wa mkutano huu mkubwa na wa kihistoria "CPC Dialogue with World Political Leaders in Africa".

Mkutano huu wa kidunia unabeba kauli mbiu isemayo nadharia na vitendo katika kutambua njia sahihi za maendeleo ambazo ni endelevu na halisia kwa nchi zetu.

Tunayo furaha na heshima kubwa kuwa na mkutano huu mkubwa Afrika na Tanzania kama sehemu ya Mpango wa kuiunganisha dunia kwa barabara na usafiri wa maji ulioasisiwa na Ndg. Xi Jinping Katibu Mkuu wa CPC na Rais wa China amesema Bi. Wang Ke.

Tunataka kujifunza zaidi kutoka China na hasa namna ya kujipanga kimkakati katika kushughulika na kuendeleza mapambano dhidi ya dhuluma na unyonyaji ili nchi yetu iinuke na kuleta manufaa makubwa kwa watu wetu wa Tanzania.

Ndg. John Pombe Joseph Magufuli, Mwenyekiti wa CCM na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania anayo kazi ya kujenga uchumi utakaowezesha kujitegemea, uchumi wa kitaifa, uchumi utakaowaondoa watanzania kutoka katika maisha ya umasikini kama China na kwa msingi huu kama Chama na Ilani tumejitambulisha kuhudumia wanyonge na kushughulika na shida za watu amesema Ndg. Bashiru Ally Kakurwa Katibu Mkuu wa CCM

Huu ni mwendelezo wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) kuimarisha mahusiano ya ndani na ya nje katika eneo la siasa, diplomasia na uchumi.

Imetolewa na:
IDARA YA ITIKADI NA UENEZI
CHAMA CHA MAPINDUZI (CCM)
OND LUMUMBA
Tags

Top Post Ad

Below Post Ad