MMILIKI wa Shule ya Sekondari ya Wasichana, John The Baptist Ajiua Kwa Kujipiga Risasi


MMILIKI wa Shule ya Sekondari ya Wasichana, John The Baptist, iliyoko Boko, Ndibalema Mayanja (64), mkazi wa Mbezi Afrikana jijini Dar es Salaam, imedaiwa amejiua kwa kujipiga risasi kifuani.

Tukio hilo lilitokea juzi asubuhi nyumbani kwake.

Kamanda wa Polisi wa Mkoa wa Kinondoni, Jumanne Murilo, aliliambia Nipashe jana kuwa Mayanja ambaye ni Kapteni mstaafu wa Jeshi la Wananchi Tanzania (JWTZ), alijiua kwa bastola aina ya Shotgun aliyokuwa anaimiliki.

“Mayanja alikuwa anasumbuliwa na ugonjwa wa saratani kwa muda wa miaka 15 na mara kwa mara kwa mujibu wa familia yake, alikuwa akitamka kwamba anataka kujiua, jana (juzi) majira ya saa tatu asubuhi akiwa nyumbani aliomba apelekewe silaha aisafishe,” alisema na kuongeza.

“Wakati akisafisha silaha yake hiyo alikuwa akitania kuwa atazisalimisha polisi silaha zake mbili anazomiliki kwa sababu muda wa kuzimiliki umeisha, alipomaliza katika hali ambayo haikutarajiwa alijielekezea kifuani na kujipiga risasi,” alisema Kamanda Murilo.

Wakati polisi ikitoa maelezo hayo, msemaji wa familia hiyo Steve Gumbo, alisema kuwa Mayanda alijipiga risasi kwa bahati mbaya wakati anasafisha silaha zake.

Alisema aliomba apatiwe silaha zake azisafishe kwa maelezo kuwa anataka kuzisalimisha polisi kwa kuwa hakuwa anazihitaji tena.

“Wakati mzee anasafisha moja ya silaha zake kulikuwa na risasi chemba na kwa bahati mbaya ilijifyatua na kumpiga kifuani na wakati akikimbizwa hospitali alifariki dunia,” alisema Gumbo.

Marehemu Mayanga alizaliwa Julai 7, mwaka 1954 na ameacha mke na watoto sita. Kwa mujibu wa familia, marehemu anatarajiwa kuzikwa siku ya Jumanne kwenye makaburi ya Kinondoni jijini Dar es Salaam.

Post a Comment

0 Comments
* Please Don't Spam Here. All the Comments are Reviewed by Admin.

Top Post Ad

Below Post Ad