Mwenyekiti UVCCM Apandishwa Kizimbani Kwa Kusambaza Taarifa za Uongo

Mwenyekiti UVCCM Apandishwa Kizimbani Kwa Kusambaza Taarifa za Uongo
Mwenyekiti wa Umoja wa Vijana CCM (UVCCM) Wilaya ya Tarime, Godfrey Francis leo Jumatatu Julai 2, 2018 amepandishwa kizimbani katika mahakama ya hakimu mkazi wilaya ya Tarime, kushtakiwa kwa kosa la kusambaza taarifa za uwongo kwa njia ya mtandao wa kijamii.

Taarifa hizo ni kuhusu kukamatwa kwa mmiliki wa kampuni ya mabasi ya Zakaria, Peter Zakaria.

Kiongozi huyo ambaye jana alihojiwa na polisi kwa saa kadhaa amesomewa mashtaka na mwendesha mashtaka wa polisi, Kazeni Mrita.

Mbele ya hakimu mkazi Veronica Mugendi, Mrita amedai mshtakiwa amesambaza taarifa hizo mchana wa Julai Mosi, 2018 kwa kuandika kuwa Zakaria alitaka kutekwa na watu wasiojulikana ambao hata hivyo aliwazidi nguvu kwa kuwajeruhi wawili kati yao.

Francis anayetetewa na wakili Onyango Otieno ameachiwa kwa dhamana hadi Jalai 30, 2018 shauri hilo litakapotajwa.

Ametimiza masharti ya kuwa na wadhamini wawili ambao kila mmoja amesaini hati ya dhamana ya Sh2 milioni.

Tags

Top Post Ad

Below Post Ad