Serikali Yasema Haina Taarifa ya Gazeti la Mwanahalisi Kushinda Kesi Mahakamani

Wakati mkurugenzi mtendaji wa kampuni ya HaliHalisi, Saed Kubenea amesema Jumatano ijayo atachapisha nakala ya kwanza ya gazeti la Mwanahalisi baada ya kushinda kesi katika Mahakama Kuu, Serikali imesema haina taarifa na ujio huo.

Kubenea aliwaambia waandishi wa habari jana kwamba, gazeti hilo limeshinda kesi iliyofunguliwa mwaka 2017 katika Mahakama Kuu Kanda ya Dar es Salaam na uamuzi umefanyika hukumu ilitolewa Jumanne ya wiki iliyopita.

“Kama kampuni Jumatano ya wiki ijayo, tutachapisha nakala ya gazeti hilo kwa mara ya kwanza tangu lifungiwe,” alisema.

Alisema taratibu za kuomba leseni zinaendelea lakini gazeti kwa mujibu wa sheria halihitaji kusajiliwa tena badala yake, Mahakama imeamuru lifunguliwe na liendelee kuchapishwa.

Kubenea ambaye pia ni mbunge wa Ubungo (Chadema), alisema Mahakama imesema mkurugenzi wa Idara ya Habari (Maelezo) hana mamlaka yoyote siyo tu kuomba watoe maelezo ni kwa nini walichapisha habari hiyo, bali hata kuwaomba wapeleke utetezi wao.

Wakili wa Kampuni hiyo, Nashoni Nkungu, alisema uamuzi huo ulitolewa Julai 24, mwaka huu na Jaji Beatrice Mutungi.

“Mahakama katika uamuzi wake ilisema amri zilizotolewa wakati wa kulifungia gazeti ni batili, hazikufuata misingi ya kisheria na hakukuwa na haki ya usikilizwaji kwa upande wa mlalamikaji.

“Mkurugenzi wa Idara ya Habari Maelezo hana mamlaka yoyote, si tu ya kuwaomba watoe maelezo juu ya habari husika, hata ya kuwaomba walete utetezi wao.

“Na mahakama ilisema hilo si jukumu mojawapo katika yale majukumu ya Mkurugenzi wa Idara ya Habari Maelezo kama yalivyoainishwa kwenye Sheria ya Huduma za Habari,” alisema Nkungu.

Alisema hata waziri hana mamlaka ya kulifungia gazeti kama alivyofanya kwa kupitia kwa Mkurugenzi wa Idara ya Habari Maelezo.

“Mamlaka pekee ambayo anayo ni kuondoa ‘content’ ya habari ambayo inaonekana inahatarisha usalama wa taifa, kimsingi hata waziri hana mamlaka ya kufungia gazeti.

“Mahakama ilisikitishwa na kutotiliwa mkazo kwa amri ambazo zilitolewa mahakamani, kwani kulikuwa na amri zingine zilizotolewa, lakini mkurugenzi aliendelea kufanya kinyume, amekanywa kutoendelea kwenda kinyume na amri ambazo mahakama imekwishazitoa.

“Mkurugenzi wa Idara ya Habari Maelezo hana mamlaka yoyote si tu ya kuwaomba kama alivyofanya katika kesi hii, hana mamlaka yoyote ya kuandika barua kwa chombo cha habari na kukiambia kijieleze,” alisema.

Hata hivyo, mkurugenzi wa Maelezo ambaye pia ni msemaji wa Serikali, Dk Hassan Abbas alisema wao kama Serikali hawana taarifa ya hukumu hiyo.

Alisema mbali na kutokuwa na taarifa ya kushinda kesi hiyo, kuna taratibu chini ya sheria ya huduma za habari zinazotakiwa kufuatwa kabla gazeti halijachapishwa.

 “Sheria hiyo imeanza kutumika Desemba 31 mwaka 2016 ambayo inaeleza kwa namna yoyote ile hakuna gazeti litakaloruhusiwa kuchapishwa bila kuwa na leseni period (basi), ”alisema Dk Abbas.

Mkurugenzi wa Kampuni ya Uchapishaji ya Hali Halisi, Saed Kubenea, alisema wanakusudia kuwashtaki Mwanasheria Mkuu wa Serikali na aliyekuwa Naibu Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Annastazia Wambura, kwa madai kuwa wameisababishia hasara kampuni hiyo ya Sh bilioni 2.2.

Alisema uamuzi huo wa mahakama umewasaidia kuonekana mbele ya jamii kwamba hawakuwa na makosa na kudai kuna watu wana hila na gazeti lao lisionekane mtaani.

“Mahakama imethibitisha hatukuwa na hatia, hivyo tunapanga kudai fidia kwa sababu tumepata hasara zaidi ya Sh bilioni 2, tumepoteza wafanyakazi, matangazo na wadau mbalimbali tuliokuwa tukishirikiana nao.

“Tutamshtaki AG na aliyekuwa Naibu Waziri (Wambura) tutamshtaki binafsi ili iwe onyo kwa viongozi wengine wanaotumia madaraka yao vibaya,” alisema Kubenea.

Mkurugenzi huyo alisema wanatarajia gazeti hilo litaanza kuchapishwa wiki ijayo na kuwataka waandishi wa habari na vyombo vya habari wasiogope kudai haki kwani mahakama bado ziko huru na zinatenda haki.

“Mwaka 2012 tulifungiwa kwa muda usiojulikana tukaenda mahakamani gazeti likarejeshwa Septemba 2015, twendeni mahakamani tukajenge hoja.

“Tunaamini mahakama zetu bado ziko huru na zinaweza zikatenda haki, isipokuwa kuna baadhi ya watu ndani ya Serikali wana kiburi cha kutotii maamuzi ya mahakama, pengine kwa masilahi yao binafsi ama kwa kutumwa,” alisema Kubenea.

Tags

Post a Comment

0 Comments
* Please Don't Spam Here. All the Comments are Reviewed by Admin.

Top Post Ad

Below Post Ad