Tuzo za Beffta: Nani Hawa Wanaomtambua na Kutaka Kumpa Mange Kimambi Tuzo ya Wanawake na Siasa Afrika?

Mwanamitindo Mtanzania aliyebadilika kuwa mwanaharakati wa kisiasa Mange Kimambi amekuwa haangaziwi sana mitandaoni tangu kutibuka kwa maandamano ya kupinga utawala wa Rais wa Tanzania John Magufuli yaliyokuwa yamepangiwa kufanyika Aprili kutibuka.

Lakini kwa siku chache zilizopita, ameanza kuzungumziwa tena hasa mtandaoni, zaidi kutokana na taarifa kwamba ameorodheshwa kushindania tuzo ya wanawake waliowahamasisha watu zaidi katika siasa Afrika.

Taarifa zimetokana na ujumbe kwenye mtandao uliochapishwa na shirika linalojiita BEFFTA.

Beffta ni ufupisho wa Black Entertainment Film Fashion Television and Arts, (Burudani, Filamu, Mitindo, Televisheni na Sanaa ya Watu Weusi). Shirika hilo linasema huwa linaangazia maslahi ya watu weusi Uingereza, Canada, Marekani, Caribbean na barani Afrika.

Katika ujumbe wa shirika hilo Instagram, ambapo wana wafuasi 21,600, limewaorodhesha wanawake sita kushindania tuzo hiyo wanaoiita Tuzo ya Mwanamke Mhamasishaji zaidi Kisiasa Afrika.


Beffta wamewaorodhesha:

Ellen Johnson Sirleaf - Liberia

Ellen Johnson Sirleaf ni mwanasiasa nchini Liberia aliyehudumu kama rais kati ya 2006-2018. Alikuwa mwanamke wa kwanza kuchaguliwa kuwa kiongozi wa nchi barani Afrika. Aliondoka madarakani mapema mwaka huu na nafasi yake ikachukuliwa na George Weah. Ingawa uongozi wa Sirleaf ulisifiwa kwa kudumisha amani, alikosolewa kwa tuhuma za ufisadi na mapendeleo. Siku chache kabla yake kustaafu baada ya kuongoza kwa miaka 12, alifukuzwa kutoka chama chake. Alitunukiwa Tuzo ya Amani ya Nobel mwaka 2011 kwa pamoja na mwanaharakati Leymah Gbowee.

Alengot Oromait -Uganda

Proscovia Alengot Oromait ni mwanafunzi wa Chuo Kikuu Uganda ambaye pia ni mwanasiasa. Alihudumu kama mbunge wa eneo la Usuk, katika wilaya ya Katakwi kati ya 2011 na 2016. Alichaguliwa mbunge akiwa na miaka 19 pekee na kuwa mbunge wa umri mdogo zaidi kuwahi kuchaguliwa nchini humo.

Joice Mujuru -Zimbabwe

Joice "Teurai-Ropa" Mujuru ni mwanasiasa nchini Zimbabwe ambaye alihudumu kama makamu wa rais kati ya 2004-2014 baada ya kuhudumu kwa miaka kadha kama waziri. Alikuwa miongoni mwa waliotazamiwa kumrithi Robert Mugabe kabla yake kufutwa. Alihudumu pia kama makamu wa rais wa chama cha Zanu-PF.

Mange Kimambi -Tanzania

Mwanamitindo Mtanzania aliyebadilika kuwa mwanaharakati wa kisiasa Mange Kimambi amekuwa aliyepanga maandamano ya kushutumu utawala wa Rais wa Tanzania John Magufuli yaliyokuwa yamepangiwa kufanyika Aprili 26.

Diane Shima Rwigara -Rwanda

Diane Shima Rwigara ni mwanamke mfanyabiashara nchini Rwanda na mwanaharakati aliyetaka kuwania urais kama mgombea wa kujitegemea katika uchaguzi mkuu wa mwaka 2017 ambao Rais Paul Kagame alitangazwa mshindi. Alikamatwa pamoja na mamake na dadake na kushtakiwa kwa makosa ya udanganyifu na uchochezi tuhuma ambazo wameziita zenye kuchochewa na kisiasa. Wamekuwa kizuizini na kesi dhidi yao ilianza rasmi wiki hii.

Mbali Ntuli -Afrika Kusini

Mbali Ntuli mwenye miaka 30 ni mwanasiasa wa chama cha Democratic Alliance anayehudumu katika bunge la jimbo la KwaZulu-Natal. Alikuwa kiongozi wa vuguvugu la vijana wa Democratic Alliance Youth.


Tuzo hiyo ni ya aina gani?
Maswali ambayo baadhi ya watu mtandaoni wamekuwa wakijiuliza ni iwapo shirika hilo ni la kweli na iwapo tuzo yenyewe ipo.

Kwenye ujumbe wa Instagram, wameeleza sababu ambayo imewafanya 'kutoa' tuzo hiyo.

Kwamba kwa muda mrefu, mchango wa wanawake katika ufanisi katika fani mbalimbali Afrika umekuwa hautambuliwi.

Madonsela amshinda Magufuli tuzo ya Forbes
Rais Magufuli mshindi wa tuzo ya ukombozi Afrika
"Hii ni kweli zaidi hasa unapoangazia masuala muhimu kama vile siasa na maendeleo. Kinyume na wenzao wa kiume, katika mfumo tulio nao sasa, wanawake wengi wanasiasa Afrika wamelazimika kukumbana na changamoto nyingi zikiwemo za kiuchumi na unyanyapaa," wameeleza.

"Barani Afrika, hudaiwa kwamba mwanamke nafasi yake ni jikoni. Hata hivyo, wanawake wanasiasa waliofanikiwa wamekuwa wakijaribu kubadilisha hili na kudhihirisha kwamba wanawake wanaweza kufanikiwa katika siasa na kuwa viongozi wema."

Kasoro inajitokeza kwenye ujumbe unaofuata, ambapo sentensi hiyo inaonekana kutokamilika. Inasema: "Katika visa vingi, wanawake ambao wanajiingiza kwenye siasa mara nyingi...(na kukomea hapo). Wanaandika tu, Piga kura hapa #befftaawards"

Tags

Post a Comment

0 Comments
* Please Don't Spam Here. All the Comments are Reviewed by Admin.

Top Post Ad

Below Post Ad