TFF Yamtangaza Mnigeria Kuwa Kocha Mkuu wa Taifa Stars

TFF Yamtangaza Mnigeria Kuwa Kocha Mkuu wa Taifa Stars
Shirikisho la soka Tanzania (TFF) limemteua mchezaji wa zamani wa Nigeria, Emmanuel Amunike kuwa kocha mkuu wa timu ya taifa ya Tanzania, Taifa Stars kwa mkataba wa miaka miwili.

Akimtambulisha kocha huyo Jumatatu, Agosti 6, Jijini Dar es Salaam, Rais wa TFF, Wallace Karia amesema.

"Mchakato wa kumpata mwalimu wetu, hatimaye leo tumekamilisha na amekuja kusaini mkataba lakini pia kuanza kazi. Na mwalimu wetu si mwingine ni raia wa Nigeria na mchezaji wa zamani wa timu ya taifa ya Nigeria, Zamalek na Sporting Lisbon, Emmanuel Amunike".

Rais Karia ameongeza kuwa kocha huyo mpya pia ataziongoza timu za taifa chini ya miaka 23, 20 na 17, amekuja pamoja na msaidizi wake ambaye amekuwa akifanya naye kazi kwa pamoja watasaidiwa na kocha msaidizi na benchi la ufundi la hapa Tanzania.


Emmanuel Amunike alizaliwa Disemba, 25 mwaka 1970 nchini Nigeria na alianza kucheza soka katika klabu ya Julius Berger ambapo alishinda kombe la ligi kuu ya nchi hiyo kabla ya kujiunga na Zamalek SC na baadaye mwaka 1994 kujiunga na Sporting CP ya Ureno .

Mwaka 1996, Amunike alijiunga na FC Barcelona ambayo aliichezea kwa msimu mmoja kabla ya kupata majeraha ya goti ambayo yalimfanya kucheza mechi tatu pekee za ligi katika jumla ya misimu mitatu aliyoitumikia klabu hiyo. Aliuzwa katika klabu ya Albacete ya ligi daraja la pili Hispania na baadaye Busan I’Cons ya Korea Kusini na Al-Wehdat SC ya Jordan.

Katika timu ya taifa ya Nigeria, Emmanuel Amunike amecheza jumla ya mechi 27 akiifungia magoli 9, alikuwa katika kikosi kilichoshiriki michuano ya kombe la dunia 1994 nchini Marekani na katika mwaka huohuo pia aliisaidia Super Eagles kushinda kombe la mataifa ya Afrika huku akichaguliwa kuwa mchezaji bora wa mwaka wa Afrika.

Akiwa kocha, amezifundisha klabu za , Al Hazm akiwa kocha msaidizi, Julius Berger, Ocean Boys, timu ya vijana ya Nigeria U-17 na Al Khartoum SC ya Sudan.
Tags

Post a Comment

0 Comments
* Please Don't Spam Here. All the Comments are Reviewed by Admin.

Top Post Ad

Below Post Ad