Waziri Mpango "Siogopi Vitisho vya Makonda...Makontena Yapigwe Mnada"


Benny Mwaipaja, WFM, Dar es Salaam
WAZIRI wa Fedha na Mipango, Dkt. Philip Mpango, amefanya ziara ya kushitukiza katika eneo la kuhifadhia makontena-Bandari Kavu Dar es Salaam (DICD), na kukagua makontena 20 yaliyoingizwa nchini na Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Paul Makonda na kuiagiza Mamlaka ya Mapato Tanzania -TRA kuendelea na mnada wa makontena hayo ili kupata kodi ya Serikali inayokadiriwa kufikia shilingi bilioni 1.2.

Dkt. Mpango amesema kuwa kodi hiyo inadaiwa kwa mujibu wa sheria za nchi baada ya mwenye mali kushindwa kulipa kodi na kwamba amesikitishwa na vitisho vinavyotolewa na Mkuu huyo wa Mkoa na vilivyonukuliwa na baadhi ya vyombo vya habari nchini  akitumia vifungu vya Biblia kwamba yeyote atakaye nunua mzigo huo atalaaniwa.

"Sheria za nchi hazichagua sura wala cheo cha mtu, na mimi ndicho nilicho apa, kutekeleza sheria za nchi, sheria za kodi, ndiyo dhamana niliyo pewa kwahiyo Kamishna, simamia sheria za kodi bila kuyumba" alisisitiza Dkt. Mpango akitoa maelekezo kwa Kamisha wa Forodha Bw. Ben Usaje.

Alifafanua kuwa mzigo wa Samani ulioagizwa kutoka nje ya nchi hauna msamaha wa kodi na kwamba huyo aliye agiza (RC Paul Makonda) alipe kodi stahidi na asipo lipa kodi hiyo mchakato unaoendelea wa kuyapiga mnada makontena hayo uendelee.

"Napenda niwaombe viongozi wenzangu Serikalini, ni muhimu tukachuja maneno! unasema mtu anayekuja kununua samani atapata laana, tena laana ya Mungu, kwa nini tunamhusisha Mungu kwenye vitu vya namna hii" alieleza kwa masikitiko Dkt. Mpango

Dkt. Mpango alitoa wito kwa watanzania wanaotaka kununua bidhaa hizo ambazo nyingi ni vifaa vinavyoweza kutumika shuleni ama maofisini kama vile viti meza na makabati, kujitokeza bila hofu kununua mali hizo.

 Aliwaomba walimu na wanafunzi wasiwe na wasiwasi na kwamba Serikali ya Awamu ya Tano imejipambanua na kuwekeza kwenye elimu kwa kutenga zaidi ya shilingi bilioni 20 kila mwezi kulipa ada ya wanafunzi ili wasome bila kulipa ada na ina mpango madhubuti wa kuboresha miundombinu ya elimu nchi nzima ikiwemo ujenzi wa madarasa na ofisi za walimu.

"Tunawapenda na kuwathamini sana walimu wetu, asitokee mtu yeyote  akaanza kuwaambia hadithi kama vile Serikali hii inawapuuza! si kweli hata kidogo" Aliongeza Dkt. Mpango

Kwa upande wake, Kamishna wa Forodha wa Mamlaka ya Mapato Tanzania-TRA, Ben Usaje, alimweleza Dkt. Philip Mpango kwamba Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Bw. Paul Makonda, aliwasilisha maombi ya kutaka kupewa msamaha wa kodi wa makontena 36 yenye samani kutoka Diapora nchini Marekani.

Alisema kuwa kati ya makontena hayo, yaliyoingia nchini ni makontena 20 ambayo yanadaiwa kodi ya shilingi bilioni 1.2 na kwamba utaratibu kwa kumtaka Paul Makonda alipe kodi hiyo ili aruhusiwe kuyachukua makontena hayo ulifanyika kwa mujibu wa sheria na kwamba mpaka sasa hajayachukua ndio maana yanapigwa mnada.

Naye aliwatahadharisha watu wanao tumia masuala ya siasa na uongozi Serikalini kutaka kukwepa kulipa kodi a kwamba suala la kodi za samani zinaonekana ziko juu kwa sababu Bunge lilitunga sheria hiyo ili kulinda soko la ndani la samani na kuweka sheria ya kutokuwepo kwa msamaha wowote wa kodi kwenye bidhaa kama hizo.

Mwisho.
Tags

Post a Comment

0 Comments
* Please Don't Spam Here. All the Comments are Reviewed by Admin.

Top Post Ad

Below Post Ad