Khadija Omary Kopa Afunguka Skendo ya Kufumaniwa


Malkia wa mipasho Afrika Mashariki na kati, Bi Khadija Omary Kopa amedai katika vitu ambavyo hatoweza kuvisahau katika maisha ni pamoja na skendo aliyowahi kuzushiwa miaka ya nyuma kuwa amechwa na mume wake kwasababu ya kufumaniwa na mwanaume mwingine.

Khadija Kopa amebainisha hayo alipokuwa anapiga stori na BIG CHAWA kwenye PLANET BONGO ya East Africa Radio na kusema kuwa katika miaka yao palikuwa hakuna mitandao ya kijamii, lakini waandishi wa magazeti ndio walikuwa wanaongoza kwa kuwatengeneza mastaa skendo zisizokuwa na kweli ili mradi waweze kuuza bidhaa zao sokoni.

"Skendo niliyowahi kuwa nayo kubwa miaka hiyo ni kutangaziwa kuachwa (nimepewa talaka) kwa kile walichokidai nimefumaniwa. Ila kiukweli sijawahi kufamaniwa bali ni watu waliamua kuzusha hivyo ili kusudi ya kwao yawaendee. Si unajua miaka yetu palikuwa hakuna mitandao ya kijamii kama hii leo", amesema Khadija Kopa.

Pamoja na hayo, Khadija Kopa ameendelea kwa kusema kuwa "mimi sijawahi kutafuta kiki, kiki zinakuja wenyewe tu ila mwandishi anaamua kufanya vile anavyotaka, nilikuwa nakaa 'front page' katika magazeti na ilikuwa haipiti siku nikakosa kuandikwa kwenye magazeti ya burudani".

Mbali na hilo, Khadija Kopa amesema sababu kubwa ya yeye hadi dakika hii kuendelea kufanya vizuri kwenye 'game' ya muziki wa taarab ni kutokana na kujua kubadilika kutokana na mazingira.

"Biashara jinsi ilivyo unapaswa uende kwa wakati, ikija digitali nawe unaenda huko huko bila ya hivyo utapotea ndugu yangu na kubakia nyuma", amesisitiza Khadija Kopa.

Bi Khadija Omary Kopa ni miongoni mwa wasanii wakongwe kwenye muziki wa taarab ambao waliweza kuwika miaka ya zamani kwa vibao vyake vingi ambavyo hadi kizazi cha sasa bado zinaendelea kufanya vizuri.

Post a Comment

0 Comments
* Please Don't Spam Here. All the Comments are Reviewed by Admin.

Top Post Ad

Below Post Ad