Kangi Lugola: Serikali ya Tanzania Haiwezi Kuruhusu USHOGA Hata Siku Moja


Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Kangi Lugola, amesema kamwe Serikali ya Tanzania, haitaruhusu ushoga na kwamba kila kiungo kilichoumbwa na Mungu kwenye mwili wa mwanadamu kina kazi yake.

Lugola ametoa kauli hiyo bungeni leo Ijumaa Novemba 9, 2018  wakati akitolea ufafanuzi kuhusu hoja iliyotolewa na Mbunge wa Konde (CCM) Khatibu Haji aliyoitoa wakati akichangia Mapendekezo ya Mpango wa Taifa wa Maendeleo kwa mwaka wa fedha 2019/20.

Akichangia Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo ya Taifa wa 2019/20, Haji alisema “kabla ya kuanza kuchangia, naanza na utangulizi ambao ni muhimu kwa ninavyoona katika siku za karibuni kumezuka mjadala kuhusiana na ndoa za jinsia moja, tumesikia kauli za mawaziri akiwamo Kangi Lugola, na Waziri wa Mambo ya Nje (Balozi Agustino Mahiga).

“Katika kauli zao inaoneka kuna kamtego juu ya kukubaliana na jambo hili na kukinzana na jambo hili, naomba niwaambie, iwe ni mtego ama ni bahati mbaya, sisi watanzania hatutaingia katika mtego wa ushoga, Tanzania hatutaki ushoga. Iwe mmetumwa ama ni mtego watanzania hatutakubali kuingia kwenye ndoa za jinsia moja.

“Tanzania ni jamuhuri ya muungano wa Tanzania, ni muungano wa serikali za Zanzibar na Tanganyika, na Zanzibar asilimia 95 ni waislamu, waislamu kwa vyovyote suala la ushoga hawatalikubali. Nawaambia nyoosheni maneno, nchi yetu hikubali ushoga na huo ndio msimamo wa watanzania.

“Nadhani mmenielewa, naumia sana moyoni mwangu kuona nchi iliyostaarabika yenye utamaduni wetu wa asili, leo kuna baadhi ya watu wanasingizia misaada iwe ajenda ya kututoa sisi kutupeka kwenye ubaradhuri, haiwezekani.

“Hili jambo ni baya na watanzania hawataki kabisa, naomba viongozi wetu mkae kimia kama hamuwezi, leo kuna Mawe ya chuma kule Liganga, hivi kwanini tusitumie akili zetu na vitu alivyotupa Mungu mpaka tunafikiria kulainisha maneno mara hatutawanyanyasa, hatutawanya hivi, watanyanyaswa kwasababu sheria yetu haikubali ushoga.


Baada ya kauli hiyo, Kangi aliomba kutoa taarifa ambapo alisema “naomba nimpe taarifa Hatibu, kwamba Bunge hili kwa mfano tunapokuwa tumekaa kupitisha bajeti, huwa tunatenga fedha kwa matumizi mbalimbali, maji, barabara, afya.

“ Lakini kuna wakati tunaweza kuzibadilishia matumizi, fedha labda za maji ziende kwenye barabara au za afya ziende kwenye maji, lakini hawa mashoga anaowazungumzia ambao ni binadamu wenye viungo mbalimbali vya mwili.

“Viungo ambavyo mashoga wanavitumia, vina matumizi kazi maalumu kwa mujibu wa uumbaji wa Mungu, Serikali yetu kamwe haitaruhusu mwanadamu yeyote kubadili matumizi ya kiungo ambacho kimesudiwa kwa ajili ya kutolea haja kitumike katika matumizi mengine ambayo Mungu hakuyakusudia.

“Kwa hiyo nimpe taarifa kwamba Serikali ya Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania inayoongozwa na John Pombe Magufuli, kwanza tuna sheria yetu ya kanuni ya adhabu ambayo inazuia kubadilisha matumizi ya kiungo cha binadamu.

“Kwa hiyo asisema labda serikali inajichanganya kwenye jambo hili, ni maelekezo ambayo tunatoa labda vyombo vinaripoti tofauti, lakini Serikali yetu kamwe, Tanzania ni hekalu la roho mtakatifu. Hatuwezi kukubali hekalu la roho mtakatifu likatumika kwa mambo ambayo hayakubaliki,” alisema Lugola.

Kwa upande wake Khatib baada ya majibu hayo amesema kati ya taarifa nzuri ambazo ziliwahi kutolewa hiyo ni taarifa bora na kwamba alitegemea kauli ya kiume kama hiyo kutolewa na Kangi (Lugola).
Tags

Post a Comment

0 Comments
* Please Don't Spam Here. All the Comments are Reviewed by Admin.

Top Post Ad

Below Post Ad