Mbunge wa Mbeya Mjini, Joseph Mbilinyi ‘Sugu’ amemtaka Rais Dkt John Pombe Magufuli kufika Jijini Mbeya kwa ajili ya kutimiza baadhi ya ahadi ambazo alizitoa wakati wa Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2015 kuwa ataijenga moja ya barabara kwenye jiji hilo.
Sugu ameeleza amekuwa akitumia mikutano mbalimbali ya wananchi kumuomba Rais Magufuli kufika Jijini Mbeya ili kuzungumza na wananchi juu ya masuala mbalimbali ya shughuli za maendeleo kabla ya uchaguzi ujao.
“Hata mimi kwa kweli nataka sana Rais aje Mbeya na katika mikutano yangu mingi ya hadhara nimeomba Rais aje atembelee na Mbeya pia kwa sababu akichelewa sana watasema anakuja kwa vile muda wa uchaguzi umekaribia.” Amesema Sugu.
“Nataka Rais aje kwa sababu sisi wana Mbeya zipo ahadi nyingi alizotoa wakati wa kampeni za uchaguzi mkuu 2015, alituahidi kwamba akishinda atatusaidia maendeleo ikiwemo barabara ya Mapelele ambayo imekuwa ni kero kubwa sana kwa wananchi,” aliongeza.
Awali Mbunge huyo alifika katika Shule ya Msingi Mabatini kwa ajili ya kukabidhi vifaa vya ujenzi wa vyoo.