Polisi Jijini Mwanza Yaua Majambazi Watatu Usiku Wa Manane

Polisi Jijini Mwanza Yaua Majambazi Watatu Usiku Wa Manane
Jeshi la Polisi Mkoa wa Mwanza, limeua watu watatu kwa tuhuma za ujambazi.

Inadaiwa watu hao walikuwa na silaha ya moto ambayo haijafahamika ni ya aina gani katika maeneo ya Nyakabungo Kata ya Isamilo wilayani Nyamagana.

Kaimu Kamanda wa jeshi hilo mkoani hapa, Advera Bulimba, alithibitisha kuuawa kwa watuhumiwa hao, huku akifafanua kuwa wengine watatu wanasadikika kutokomea kusikojulika.

Tukio hilo lilitokea  juzi majira ya saa nane usiku, baada ya askari kupokea taarifa toka kwa raia wema kuwa katika maeneo hayo kunasikika milio ya risasi ambayo ilikuwa inaashiria kuwapo kwa uvunjifu wa amani.

Bulimba alisema baada ya taarifa hiyo kuwafikia askari waliokuwa doria, walifuatilia na kufika eneo la tukio haraka baada ya watuhumiwa kuhisi uwapo wa polisi walianza kujihami kwa kuwarushia risasi na kuanza kujibizana na kufanikiwa kuwaua watatu.

“Majambazi hao hawakufanikiwa kuiba mali yoyote wala kusababisha madhara kwa wananchi, na miili yao imehifadhiwa katika Hospital ya mkoa Sekou-Toure kwa uchunguzi na utambuzi, na baada ya kukamilika itakabidhiwa kwa ndugu wa marehemu kwa ajili ya mazishi,” alisema Bulimba.

“Tunawaomba wananchi kuendelea kutupatia ushirikiano wa taarifa za viashiria vya uhalifu mapema ili tuweze kuwakamata wahusika na kuwafikisha kwenye vyombo vya sheria," alisema Bulimba.

Tukio hilo ni mwendelezo wa makabiliano ya polisi na watuhumiwa wa ujambazi. Januari mwaka huu watuhumiwa wanane wa ujambazi waliuawa na jeshi hilo kisiwani Ukerewe.

Post a Comment

0 Comments
* Please Don't Spam Here. All the Comments are Reviewed by Admin.

Top Post Ad

Below Post Ad