Kamati ya Bunge Yaridhishwa na Ukarabati wa Chuo Kikuu cha Ardhi

Kamati ya Bunge Yaridhishwa na Ukarabati was Chuo Kikuu Ardhi
Ndalichako na Mjumbe wa Kamati ya Bunge ya Kudumu ya Huduma na Maendeleo ya Jamii, Suzan Lyimo, wakifuatilia taarifa iliyowasilishwa na Makamu Mkuu wa Chuo Kikuu Ardhi, Prof. Evaristo Liwa (hayupo pichani)  wakati kamati hiyo ilipofanya ziara ya kukagua maendeleo ya utekelezaji wa mradi  wa ukarabati na upanuzi wa miundombinu ya chuo hicho.

Naibu Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, Wiliam Ole Nasha,  akiwaonyesha wajumbe wa kamati  hiyo madarasa yanayoendelea kukarabatiwa (hayapo pichani) wakati kamati hiyo ilipofanya ziara katika chuo hicho.


Wajumbe wakiangalia baadhi ya kazi za mipango-miji, usanifu majengo, upimaji na ramani zilizotengenezwa na wanafunzi wa chuo hicho ikiwa sehemu ya mafunzo kwa vitendo.
Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, Ndalichako akimkabidhi Kaimu Mwenyekiti wa Kamati ya Bunge ya Kudumu ya Huduma na Maendeleo ya Jamii, Oscar Mukasa, machapisho ya chuo hicho.

KAMATI ya Kudumu ya Bunge ya Huduma na Maendeleo ya Jamii imeipongeza serikali kwa kutoa fedha kiasi cha shilingi bilioni 2.5 za mradi wa ukarabati na upanuzi wa miundombinu ya Chuo Kikuu Ardhi zilizotengwa katika bajeti ya mwaka 2018/19.



Pongeza hizo zimetolewa na Kaimu Mwenyekiti wa Kamati hiyo, Oscar Mukasa, jijini Dar es salaam baada ya kukagua utekelezaji wa mradi wa ukarabati na upanuzi wa miundombinu hiyo ambayo ni ujenzi wa maabara, ukarabati wa karakana, nyumba za walimu, madarasa na kukamilisha ujenzi wa jengo la Lands.



Aidha,  Mukasa pamoja na kamati wameipongeza Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia kwa kusimamia utekelezaji wa mradi kwa ubora na weledi mkubwa. Vilevile wamepongeza chuo hicho kwa kutumia vyema wataalamu wake kwenye kutekeleza kazi ya ujenzi.

Katika hatua nyingine, kamati imeshauri serikali kutoa kipaumbele cha kukiendeleza kituo cha utoaji taarifa za viashiria vya majanga yanayoweza kusababishwa na volcano na matetemeko ya ardhi katika eneo la Oldonyo Lengai. Aidha wameishauri serikali kuhakikisha kituo kinapata vifaa vitakavyokiwezesha kufanya kazi ya kutambua viashiria hivyo katika maeneo yote ya nchi na kutoa taarifa hizo.



Awali Makamu Mkuu wa Chuo Kikuu Ardhi, Prof. Evaristo Liwa, akitoa taarifa ya utekelezaji kwa kamati amesema mradi huo unaogharimu Shilingi bilioni 2.5 kwa kiasi kikubwa umesimamiwa na wataalamu wa ndani ya chuo,  hali ambayo imewezesha kupunguza gharama na ameishukuru serikali kwa kutoa fedha kwa wakati.



Naye Waziri Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, Prof. Joyce Ndalichako, ameishukuru kamati hiyo kwa kutembelea mradi na ameahidi kusimamia kwa ukaribu utekelezaji wa maelekezo yaliyotolewa na kamati.



Imetolewa na Kitengo cha Mawasiliano Serikalini Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia.


Post a Comment

0 Comments
* Please Don't Spam Here. All the Comments are Reviewed by Admin.

Top Post Ad

Below Post Ad