Msichana wa Kazi Aiba MTOTO wa Mwaka Mmoja Akamatwa Tabora


Picha si ya tukio
Mfanyakazi wa ndani, Christina Claudia (23) anashikiliwa na polisi mkoani Morogoro kwa tuhuma za kuiba mtoto mwenye umri wa mwaka mmoja wilayani Kilosa na kukimbia naye mkoani Tabora.

Akizungumza na waandishi kuhusiana na tukio hilo, Kamanda wa polisi mkoani Morogoro, Wilbroad Mutafungwa amesema mtoto huyo aliibiwa Juni 25, 2019 majira ya saa 3 asubuhi huko kitongoji cha Manzese A kata ya Mkwatani wilayani Kilosa.

Amesema msichana huyo anadaiwa kumdanganya Mariet Deogratius (16) ambaye ni dada wa mtoto huyo (Thomas Deogratius mwenye mwaka mmoja) aliyeibiwa kuwa anaenda naye kufua nguo bombani ndipo alipopata upenyo na kutoroka naye.

Amesema mama wa mtoto huyo Flora Thomas (32) alikuwa kazini na ilipofika muda wa saa 6 mchana aliagiza mtoto wake apelekewe anakofanyia kazi ili aweze kumnyonyesha kwani amekuwa akifanya hivyo mara kwa mara ndipo aliambiwa mtoto huyo alitoka na dada huyo.

Mutafungwa amesema baada ya kukaa muda mrefu bila msichana huyo kurudi ndipo walipoamua kutoa taarifa kituo cha polisi Kilosa na kuanza kufutilia.

Amesema walifanikiwa kumkamata dada huyo wa kazi Juni 29, 2019, katika kijiji cha Mwakabasa, kata ya Mahonda wilaya Nzega mkoani Tabora akiwa na mtoto huyo.

Kamanda huyo amesema mtoto huyo tayari amekabidhiwa kwa wazazi wake akiwa salama na kwa sasa anafanyiwa uchunguzi wa kiafya kubaini kama amepatwa na madhara yoyote.

Kamanda alisema msichana huyo wa kazi anashikiliwa na polisi kwa uchunguzi zaidi na kufahamu alikuwa na nia gani kwa mtoto huyo na atafikishwa mahakamani wakati wowote mara baada ya uchunguzi kukamilika.

Post a Comment

0 Comments
* Please Don't Spam Here. All the Comments are Reviewed by Admin.

Top Post Ad

Below Post Ad