Chama, Nyoni Wafumua Kikosi Simba


BEKI mkongwe ndani ya Simba, Erasto Nyoni na viungo Clatous Chama na Sharraf Eldin Shiboub hawatakuwa sehemu ya kikosi cha timu hiyo kitakachoivaa Ruvu Shooting leo.



Timu hizo leo zinatarajiwa kujitupa kwenye Uwanja wa Uhuru jijini Dar es Salaam katika mchezo wa Ligi Kuu Bara utakaopigwa kwenye uwanja huo wenye nyasi bandia.



Kwa mujibu wa kocha mkuu wa timu hiyo Mbelgiji, Patrick Aussems wachezaji hao watakosekana kwa sababu mbalimbali ikiwemo ya majeraha ambayo anayo Shiboub anayeuguza majeraha ya misuli, Nyoni yeye goti na Chama alichelewa kujiunga na timu akitokea kwenye majukumu ya timu ya taifa ya Zambia.


Clatous Chama

Wakati wachezaji hao wakikosekana tayari kocha huyo amewaandaa wachezaji wengine watakaochukua nafasi zao ambao amewapa mbinu za kuhakikisha wanapata ushindi.



Katika mazoezi ya mwisho yaliyofanyika jana asubuhi kwenye Uwanja wa Gymkhana, Posta , Dar kocha huyo alionekana kuwandaa mabeki wawili wa kati kwa wakati tofauti ambao ni Mbrazili, Tairone Dos Santos na Kennedy Juma ili mmoja wao achukue nafasi ya Nyoni.



Akiendelea kuwandaa mabeki hao Muivory Coast, Serge Wawa ndiye alikuwa anabadilishiwa mabeki hao wawili ambao mmoja wao atacheza naye pamoja katika mchezo huo dhidi ya Ruvu.



Katika hatua nyingine, kocha huyo alionekana kuwaongezea mbinu viungo wake washambuliaji Hassani Dilunga na Francis Kahata watakaocheza nafasi za Shiboub na Chama katika mchezo huo.



Kikosi cha Simba kinachotarajiwa kucheza na Ruvu kinatarajiwa kuwa hivi; Kipa ni Aishi Manula, Shomari Kapombe, Mohammed Hussein ‘Tshabalala’, Tairone, Wawa, Gerson Fraga, Kahata, Mzamiru Yassin, Kagere, Miraji Athumani ‘Sheva’ na Dilunga.



Akizungumzia mchezo huo, Aussems alisema kuwa: “Tayari nimekamilisha maandalizi kuelekea mchezo huo na kikubwa tunahitaji pointi tatu ili tuendelee kukaa kileleni.



“Uzuri ninawafahamu vizuri wapinzani wangu Ruvu, siyo timu ndogo ni kubwa inayoweza kupata matokeo mazuri, hivyo sitawadharau tutakapokutana hiyo kesho (leo),” alisema Aussems.

Post a Comment

0 Comments
* Please Don't Spam Here. All the Comments are Reviewed by Admin.

Top Post Ad

Below Post Ad