Rais Magufuli Achagia Milioni 5 Kwa Ajili ya Ujenzi wa Nyumba ya Padre


Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. John Pombe Magufuli tarehe 08 Desemba, 2019 ameungana na Waumini wa Parokia ya Epiphania Bugando Jijini Mwanza kusali Misa Takatifu ya Dominika ya 2 ya Majilio iliyoongozwa na Askofu Mkuu wa Jimbo Kuu Katoliki la Mwanza Mhashamu Renatus Nkwande.

Katika mahubiri yake, Baba Askofu Mkuu Nkwande amesema sawia na kipindi hiki cha Majilio ambapo Wakristo wanakumbushwa kufanya toba na kufanya matendo mema, Watanzania wanapaswa kujitafakari juu ya matendo yao na kuachana na matendo yamchukizayo Mwenyezi Mungu yakiwemo mauaji, wizi na ubinafsi.

Baba Askofu Mkuu Nkwande amesema inasikitisha kusikia wapo baadhi ya Watanzania wanaoiba na kujilimbikizia mali, ilihali Watanzania wenzao wanapata taabu kwa ukosefu wa huduma za kijamii kutokana na rasilimali nyingi kukumbatiwa na watu wachache.


Amemuombea Mhe. Rais Magufuli na viongozi wote Serikali kuendelea kutekeleza majukumu yao vizuri kama ambavyo wameanza, na amempongeza Mhe. Rais Magufuli kwa kuhimiza watu kufanya kazi, kuwa waadilifu na kuacha wizi.

“Mhe. Rais jipe moyo, endelea na kazi hiyo kwa sababu Watanzania tunafurahia unachokifanya na tunakuunga mkono” amesema Baba Askofu Mkuu Nkwande.

Katika salamu zake, Mhe. Rais Magufuli ambaye alisali katika Kanisa hilo kwa mara ya mwisho mwaka 1978 akiwa kidato cha nne, amemshukuru Baba Askofu Nkwande kwa mahubiri mazuri yanayohimiza kuepuka dhambi na kutenda yaliyo mema na amewataka Watanzania kuzingatia ujumbe huo.

Mhe. Rais Magufuli ambaye ameongozana na Mkewe Mama Janeth Magufuli amechangia shilingi Milioni 5 kwa ajili ya ujenzi wa nyumba ya Padre wa Parokia hiyo na ameongoza harambee iliyofanikisha kupatikana kwa shilingi 12,650,000/= kwa ajili ya ujenzi huo.
Tags

Post a Comment

0 Comments
* Please Don't Spam Here. All the Comments are Reviewed by Admin.

Top Post Ad

Below Post Ad