Polisi 27 wa Sudan wahukumiwa kifo kwa hatia ya kumuua mwalimu



Mahakama nchini Sudan imewahukumu adhabu ya kifo maafisa 27 wa polisi baada ya kupatikana na hatia ya kumtesa na kumuua mwalimu, Ahmad al-Khair.

Polisi hao wamepatikana na hatia ya kumuua mwalimu Ahmad al-Khair, 36, aliyeaga dunia kutokana na mateso makali baada ya kukamatwa wakati wa maandamano ya kumuondoa madarakani rais wa zamani wa Sudan, Omar al-Bashir.

Mahakama ya Sudan pia imewahukumu vifungo watuhumiwa wengine 13 na kuwaachia huru wengine 4 baada ya kupatikana kuwa hawana hatia.

Mahakama hiyo imesema Ahmad Al-Khair alipigwa na kuteswa hadi kufa na maafisa wa polisi wakati alipokamatwa na kupelekwa kwenye eneo la utesaji katika jimbo la Kassala.

Mauaji ya mwalimu Ahmad al-Khair yalichochea zaidi maandamano ya wananchi wa Sudan dhidi ya utawala wa Omar al Bashir na hatimaye tarehe 11 Aprili mwaka huu, jeshi la Sudan lilimng'oa madarakani rais huyo wa zamani aliyeingia madarakani kwa mapinduzi ya kijeshi na kuitawala Sudan kwa takriban miaka 30.

Hukumu ya  kifo iliyotolewa na mahakama ya Sudan dhidi ya idadi hiyo kubwa ya maafisa wa polisi inahesabiwa kuwa ya aina yake kwa kuzingatia kuwa chombo hicho kilikuwa na nguvu kubwa sana katika kipindi cha utawala wa Omar al Bashir.

Takribani watu 170 waliuwawa wakati wa maandamano dhidi ya Serikali yake.

Al Bashir pia anasakwa na Mahakama ya Kimataifa ya Jinai (ICC) kwa tuhuma za kufanya uhalifu na jinai za kivita dhidi ya raia wa Darfur huko magharibi mwa Sudan.

Tags

Post a Comment

0 Comments
* Please Don't Spam Here. All the Comments are Reviewed by Admin.

Top Post Ad

Below Post Ad