"Kagere si Mchezaji wa Majaribio, Nimewakatalia Levante " - Wakala

 
Wakala wa mshambuliaji Meddie Kagere wa klabu ya Simba na timu ya taifa ya Rwanda, aitwaye Patrick Gakumba amesema kuwa hivi sasa amepokea ofa kutoka klabu nyingi kuhusu mchezaji wake, ikiwemo klabu ya Levante ya Hispania.


Akizungumza kupitia Kipenga ya East Africa Radio, Gakumba amesema kuwa katika kipindi hiki ambacho yupo kwenye mazungumzo ya mchezaji wake kuongeza mkataba na Simba, klabu ya Levante imejitokeza kuonesha nia ya kumhitaji mshambuliaji huyo lakini imemtaka kwa majaribio, kitu ambacho wakala huyo amesema hakiwezekani akisema kuwa mchezaji wake si wa majaribio.

"Levante wameniambia Kagere walimuona kupitia Sevilla walipokuja kucheza na Simba Tanzania, lakini tumeshindwana kidogo tu kwa sababu wao wanataka akacheze kwanza mechi za majaribio, lakini nimewaambia Kagere si mchezaji wa majaribio", amesema Gakumba.

"Mimi nawaambia Kagere atacheza mpaka hao watoto wadogo wanaomuita ni mzee watachoka, kwa sababu walianza kumsema mzee tangu miaka 5 iliyopita nyuma lakini kila wakimsema anafunga", ameongeza.

Aidha Gakumba amesema kuwa Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi wa Simba, Mohammed Dewji 'Mo' ana nia ya kumbakiza mshambuliaji huyo, hivyo wako katika mazungumzo na mashabiki watajua baadaye kama atabakia au ataondoka.
Tags

Post a Comment

0 Comments
* Please Don't Spam Here. All the Comments are Reviewed by Admin.

Top Post Ad

Below Post Ad