WHO yahofia Corona Kuiumiza Afrika, Yakadiria Vifo na Ongezeko la Umasikini


Shirika la Afya Duniani (WHO) limetahadharisha kuwa huenda Afrika ikageuka kuwa kituo cha kusambaa kwa maambukizi mapya ya virusi vya corona (covid-19) endapo hatua sitahiki hazitachukuliwa.

Kwa mujibu wa maafisa wa Umoja wa Mataifa, inakadiriwa kuwa virusi hivyo vinaweza kusababisha vifo vya watu 300,000 na kusababisha ufukara kwa watu takribani milioni 30.

Imeripotiwa kuwa hadi sasa kuna takribani vifo 1,000 na maambukizi 19,000 barani Afrika. Ingawa ni chini ya kiwango kilichorekodiwa kwa bara la Ulaya na Marekani, tahadhari imetolewa zaidi kwa Afrika kutokana na mazingira halisi ya mifumo ya afya.

Tume ya Umoja wa Mataifa ya Uchumi ambayo pia imetahadharisha kuwa watu 300,000 wanaweza kupoteza maisha, imependekeza Afrika ipewe msaada wa vifaa vyenye thamani ya $100 bilioni pamoja na kuipunguzia madeni ya nje.

WHO wameeleza kuwa maambukizi ya virusi vya corona hivi sasa vinaanza kusambaa kwa kasi nje ya miji mikuu na majiji muhimu barani humo.

Zaidi ya theluthi ya wakaazi wa bara la Afrika wanakabiliwa na uhaba wa huduma ya maji safi na salama, na zaidi ya 60% ya wakaazi wa mijini wanaishi kwenye maeneo yenye msongamano ambayo yanaweza kuwa hatari zaidi kwa maambukizi ya virusi vya corona endapo hatua stahiki hazitachukuliwa.

Afrika Kaskazini ndio eneo lililotajwa kuathirika zaidi katika bara hilo. Algeria, Misri na Morocco ina visa zaidi ya 2,000 vya corona na vifo takribani 100. Algeria ndio nchi inayoongoza kwa vifo vitokanavyo na corona, ambavyo ni 348.
Tags

Post a Comment

0 Comments
* Please Don't Spam Here. All the Comments are Reviewed by Admin.

Top Post Ad

Below Post Ad