Zitto Kabwe Hakubali Kushindwa..Unaambiwa Kaandika Barua Nyingine, Sasa Aitaka IMF Kuikagua BOT


KIONGOZI wa Chama cha ACT-Wazalendo, Zitto Kabwe ameeleza kuwa ameliandikia barua Shirika la Fedha la Kimataifa (IMF), kulitaka kuja nchini kuifanyia ukaguzi Benki Kuu (BoT), kutokana na kuwa na mashaka ya ukaguzi uliofanywa na Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa hesabu za serikali (CAG).
Zitto ameyasema hayo leo tarehe 11 Aprili 2020, wakati akihutubia kupitia vyombo vya habari vya mtandao ambapo ametanabaisha kuwa kutokana na kashfa ya wizi wa fedha za EPA Serikali, Benki Kuu, Bunge na CAG walikubaliana kuwa Benki Kuu inapaswa kukaguliwa na chombo huru kwa niaba ya CAG.

Soma hotuba kamili ya Zitto ya uchambuzi huo wa CAG

UCHAMBUZI WA RIPOTI ZA MDHIBITI NA MKAGUZI MKUU WA HESABU ZA SERIKALI WAKATI YA UTAWALA WA AWAMU YA TANO CHINI YA RAIS JOHN POMBE MAGUFULI

UTANGULIZI
Ndugu zangu, Watanzania wenzangu, leo tarehe 11 Aprili, 2020 siku moja kabla ya Sikukuu ya Pasaka, siku ambayo kwa ndugu zetu Wakristo kote ulimwenguni ni siku muhimu na yenye kuleta tafakari kwa ustawi wao kiimani, nimeona niitumie kuwasilisha uchambuzi wa Chama chetu, ACT Wazalendo, chama ambacho kimeendelea kujipambanua kama Chama mbandala na kinachozielekeza katika kujadili masuala makubwa ya kitaifa na kupendekeza suluhu yake.

Kwa kuzingatia utamaduni wetu huo, na baada ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG) kuwasilisha Taarifa yake kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019; Sisi ACT Wazalendo, tumeisoma, kuipitia na kuichambua taarifa husika, kwa lengo la kuitumia ili itusaidie kutimiza wajibu wetu wa kuisimamia Serikali kama chama mbadala nchini na kama Chama cha Upinzani Bungeni.

Katika uchambuzi wetu wa mwaka huu, tumeona ni bora pia tufanye mapitio ya Taarifa za CAG kwa miaka yote mitano ya Serikali ya Awamu ya Tano (2015/16 – 2018/19) Hivyo, uchambuzi wetu utakuwa ni uchambuzi mtambuka tangu Serikali ya Rais Magufuli ilipoingia madarakani hadi sasa. Uchambuzi huu unaibua ukweli mmoja tu kwamba Miaka 5 ya Serikali ya Awamu ya Tano chini ya Rais Magufuli ni Miaka 5 ya kushindwa kazi, na ni Miaka 5 ya kufuja fedha za Watanzania, yaani “Five years of Incompetence”.

Kwa kuwa uchambuzi wetu umebaini masuala mengi, na kwa kuwa hatutaweza kuwa na muda wa kutosha kujadili masuala yote hayo, uchambuzi wetu umejielekeza katika masuala makubwa 10, kama ifuatavyo.

Kuporomoka kwa Makusanyo ya Kodi

Ndugu Wananchi,
Mtakumbuka tangu Serikali ya Rais Magufuli iingie madarakani imekuwa ikijinasibu kuwa kinara wa ukusanyaji kodi. Kupitia tarifa mbalimbali za TRA na Msemaji Wa Serikali, tumekuwa tukiaminishwa kwamba ukusanyaji wa mapato umeongezeka katika kipindi cha Serikali ya Awamu ya Tano.

Hata hivyo, Uchambuzi wa ACT Wazalendo kwenye Ripoti ya CAG umebaini kwamba, uwezo wa Serikali ya Magufuli wa kukusanya mapato kulinganisha na Pato la Taifa umeshuka kwa kiwango cha kutisha. Hii inapelekea Serikali kushindwa kutekeleza Bajeti iliyopitishwa na Bunge na kuifanya Bajeti kuwa haina maana.

Suala hili tumekuwa tunalizungumza kila mwaka tangu Serikali ya Awamu ya Tano iingie Madarakani. Kwenye Bajeti ya Serikali ya mwaka wa Fedha wa 2016/17 (mwaka wa kwanza kamili wa Serikali ya Awamu ya Tano), Serikali ilipanga kukusanya shilingi 29.5 trilioni, kwa mujibu wa ripoti ya CAG ya 2016/17, kati ya fedha hizo, Serikali ilikusanya shilingi 25.3 trilioni tu. Na hivyo, kutokufikia lengo la makusanyo kwa 14.33%.

Bajeti ya Pili, Mwaka 2017/18, jumla ya shilingi 31.7 trilioni zilitarajiwa kukusanywa na zilipitishwa kutumika na Bunge. Serikali iliweza kukusanya kutoka vyanzo vyake vyote shilingi 27.7 trilioni tu. Hivyo kutofikia lengo la makusanyo kwa 12.66%.

Bajeti ya Tatu, Mwaka 2018/19 Jumla ya Shilingi Trilioni 32.5 zilitarajiwa kukusanywa. Lakini kwa mujibu wa Taarifa ya CAG, Serikali ilikusanya shilingi Trilioni 25.8 tu. Hivyo kutofikia lengo la makusanyo kwa 21%. Makusanyo ya Mapato yote ya Serikali katika mwaka 2018/19 yalikuwa madogo kuliko Bajeti ya mwaka uliotangulia wa 2017/18 kwa Shilingi Trilioni 1.9, yaani chini ya 7% ya Bajeti ya Pili ya Serikali ya Awamu ya Tano. Kwa miaka 3 ya mwanzo ya Serikali ya Awamu ya Tano wastani wa lengo lisilofikiwa ni 16%.

Ukilinganisha na Serikali iliyopita, kwa miaka mitatu ya mwisho wa Serikali hiyo, wastani wa lengo lisilofikiwa na Serikali katika ukusanyaji wa mapato ya Bajeti lilikuwa ni 6.3% tu – ambapo kwa mwaka 2013/14 lengo halikufikiwa kwa 9%, kwa  mwaka 2014/15 nako lengo halikufikiwa kwa 4%, na kwa mwaka wa fedha wa 2015/16 lengo halikufikiwa kwa 6% tu.

Ndugu Wananchi,
Duniani kote ufanisi wa Taifa kukusanya kodi hupimwa kwa kutazama uwiano wa Makusanyo ya Kodi kwa thamani ya shughuli za uchumi katika nchi husika, yaani Tax/GDP Ratio kwa lugha ya kiuchumi. Wakati Serikali ya Awamu ya Tano inaingia madarakani mwaka 2015/16 Uwiano wa Makusanyo ya Kodi kwa Pato la Taifa ilikuwa ni 13.68% – Maana yake Katika shilingi 100 inayozalishwa katika Uchumi, shilingi 13.7 zilikuwa zinakusanywa na Serikali kama Mapato.
Mpango wa Maendeleo wa Taifa wa miaka Mitano, 2015/16 mpaka 2020/2021 uliweka lengo la Uwiano wa Makusanyo ya Kodi kwa Pato la Taifa kuwa 20%. Kiwango cha Juu kabisa cha kiashiria hiki kilifikiwa mwaka 2013/14 wakati wa Awamu ya Nne ambapo ilikuwa 16.9%.

Kipimo hiki cha Ufanisi kinaonyesha kuwa Serikali ya Awamu ya Tano inashindwa kukusanya kodi kulingana na ukuaji wa uchumi wa Taifa.Kwa Mujibu ya Ripoti za CAG,  Mwaka 2016/17 Uwiano wa Makusanyo ya Kodi kwa Pato la Taifa ulishuka mpaka 13.2%, mwaka 2017/18 ulikuwa 12.8% na Mwaka 2018/19 umekuwa 11.4%.Kwa kutumia kipimo hiki Tanzania inashika mkia katika EAC.

Hii ndiyo hali katika Miaka 5 ya Serikali ya Awamu ya Tano chini ya Rais Magufuli, Ni Miaka 5 ya kushindwa kazi na ni Miaka 5 ya kufuja fedha za Watanzania, yaani “Five years of Incompetence”.

Deni la Taifa linakua kwa kasi kuliko kasi ya Ukuaji wa Uchumi

Ndugu Wananchi,
Pamoja na kuporomoka kwa uwezo wa Serikali ya Magufuli katika ukusanyaji wa kodi, Serikali hiyo pia imeendelea kupalilia ukuaji wa deni la Taifa. Serikali ya Awamu ya Tano iliingia madarakani Deni la Taifa likiwa ni Shilingi Trilioni 33.5 Mwezi Juni, 2015. Deni hilo liliongezeka kwa 22% kufikia Shilingi Trilioni 41 ilipofika Mwezi Juni, 2016.

Katika ukaguzi wa CAG wa mwaka 2015/16, alionyesha kuwa mikopo ya Biashara yenye riba kubwa na muda mfupi wa kuiva kabla ya kulipa iliongezeka kwa kasi zaidi ndani ya muda mfupi. Kati ya Juni 2015 na Juni 2016 MIkopo ya Biashara iliongezeka kwa 31%. Vile vile CAG alionyesha kuwa Serikali ilikopa katika soko la ndani 42% ya kiwango ilichopaswa kukopa na hivyo kusababisha madhara makubwa kwenye uchumi ikiwemo mzunguko wa Fedha kuporomoka na kusabaibsha hali ngumu ya maisha ya wananchi.

Mwaka 2016/17 mwenendo wa Deni la Taifa uliendelea kuwa ule ule ambapo Deni liliongezeka kwa 12% kufikia Shilingi Trilioni 46. Serikali iliendelea kukopa zaidi ya kiwango kwenye soko la ndani ambapo dhamana za Serikali ziliongezeka kwa 26% zaidi ya kiwango kilichoruhusiwa na Bunge katika Bajeti.

Vilevile, mwaka 2016/17 CAG alieleza kuwa Serikali ilikopa zaidi ya kiwango kinachotakiwa kutoka Benki Kuu ya Tanzania kwa jumla ya Shilingi Trilioni 1.5 na kusababisha riba ya mkopo huu kuzidi kwa 269% kufikia shilingi 157 bilioni. Suala kama hili lilitokea katika ukaguzi wa mwaka 2015/16 ambapo Serikali ilichota fedha Shilingi Bilioni 441 kutoka Benki Kuu kinyume cha sheria na kuficha mkopo huo (hidden loan) wakaguzi wasione.

Mwaka 2017/18 mwenendo wa Deni la Taifa uliendelea kukua kwa tarakimu mbili ambapo Deni liliongezeka kwa 11% kufikia Shilingi Trilioni 51. Mwaka 2017/18 Serikali ilianza kushindwa kulipa Deni la ndani kutoka kwenye mauzo ya hati fungani kama ambavyo imekuwa kawaida ya miaka ya nyuma. Mwaka huu Serikali ilipaswa kulipa madeni yenye thamani ya Shilingi Trilioni 6.1 lakini kutoka kwenye soko la ndani iliweza kukusanya shilingi Trilioni 5.7 tu. Mwenendo wa Serikali kuvunja sheria ya Benki Kuu kwa kukopa zaidi ya kiwango na kujaribu kuficha deni iliendelea ambapo shilingi 212 bilioni zilichotwa kutoka Benki Kuu katika mwaka huu wa Fedha wa 2017/18.
Mwaka huu ambao tunafanyia uchambuzi, Deni la Taifa limefikia Shilingi Trilioni 53 ilipofika Juni 2019, deni lilikuwa kwa 4% tu kutokana na kukosekana kwa mikopo ndani na nje ya nchi kufuatia hali mbaya ya Uchumi ambayo ni zao la maamuzi ya Serikali. Tutaona hili pia kwenye suala la makusanyo ya kodi.

Ukuaji huu wa deni la Taifa, haujawahi kushuhudiwa tangu nchi hii imeasisiwa, na sisi ACT Wazalendo tumekuwa tukitilia mashaka mwenendo wa ukuaji wa deni hilo. Uchambuzi wetu unaonyesha kuwa Deni la Taifa limekuwa kwa wastani wa 12.25% kwa mwaka kati ya mwaka 2015/16 – 2018/19.  Wakati deni hilo likiumuka hivyo, chini ya Serikali ya Rais Magufuli, ukuaji wa Pato la Taifa la Tanzania (GDP) umekua kwa wastani wa 6% tu, yaani, deni la Taifa limekuwa mara mbili zaidi ya ukuaji wa Pato la Taifa.

Kutokana na kukua kwa kasi kwa Deni la Taifa kiwango cha Bajeti kwa ajili ya kuhudumia Deni (kulipa deni na riba) kimeongezeka kwa kutoka Shilingi Trilioni 6.3 Mwaka 2015/16 hadi Shilingi Trilioni 10 mwaka 2018/19. Kwa vyovyote vile, hali hii ndiyo inayosababisha “vyuma kukaza”.

Hii ndiyo hali katika Miaka 5 ya Serikali ya Awamu ya Tano chini ya Rais Magufuli, Ni Miaka 5 ya kushindwa kazi na ni Miaka 5 ya kufuja fedha za Watanzania, yaani “Five years of Incompetence.”
Tags

Post a Comment

4 Comments
* Please Don't Spam Here. All the Comments are Reviewed by Admin.
  1. Wala msimjibu huyu MZAMIAJI.
    Mtafuta kiki Dakika za Majeruhi..
    Kilaza wa kopy paste huko twitter na...
    Mdandia mada bila kujuaChimbuko yupoX2

    Sasa mie NAMPOTEZEA.
    HANA LAKE JAMBO. Mil500 TZ.tumezipata.

    Kitabu chetu cha kusafiria unakirudisha kwa mama Makekele haraka by 30 Jun.

    ReplyDelete
    Replies
    1. INAONESHA UAMUZI WA MKPO TOKABENKI YADUNIA, MEMCHENGUA DOGOOO..!!

      Sasa anata kujinasibu kwa mjomba gani..??

      Hii ndio balaa ya kujifungia kibandani peke yako.hv kalantini

      Delete
  2. Wala msimjibu huyu MZAMIAJI.
    Mtafuta kiki Dakika za Majeruhi..
    Kilaza wa kopy paste huko twitter na..Fezibook na tik tok na tecno phone

    Mdandia mada bila kujuaChimbuko yupoX2

    Sasa mie NAMPOTEZEA.
    HANA LAKE JAMBO. Mil500 TZ.tumezipata.

    Kitabu chetu cha kusafiria unakirudisha kwa mama Makekele haraka by 30 Jun.

    ReplyDelete
    Replies
    1. Swadakta Mdau.

      Kibaraka atajitahidi siku zote kuwaridhisha Mabeberu apate ujira.

      Delete

Top Post Ad

Below Post Ad