Rekodi, Kisasi Mapinduzi Cup Simba dhidi ya Azam



USIKU wa leo Alhamisi saa 2:15 usiku, Uwanja wa Aman uliopo hapa Unguja, Zanzibar, utashuhudiwa mchezo mmoja wa fainali ya Kombe la Mapinduzi kati ya Simba dhidi ya Azam.

 

Simba wametinga fainali baada ya kuwatoa Namungo kwa kuwafunga mabao 2-0, huku Azam wakiwafunga Yanga kwa penalti 9-8 baada ya mechi kwenda dakika 90 kwa suluhu.


Hii ni fainali ya nne kwenye historia ya michuano ya Mapinduzi Cup kuzikutanisha Simba na Azam FC ambapo
fainali tatu zilizopita, Azam FC ilishinda zote.



Azam ndiyo timu pekee iliyobeba taji hilo mara nyingi zaidi ambazo ni tano, huku Simba wakilibeba mara tatu.
Mchezo huu wa leo ni wa kisasi na rekodi kwa sababu Simba watakuwa wanataka kufuta uteja wa kufungwa na Azam
kwenye fainali zote tatu, hukuAzam wakitaka kuendeleza rekodi yao nzuri kwa Simba na kubeba taji la sita.


Kuelekea mchezo huo, Mkuu wa Idara ya Habari na Mawasiliano wa Azam FC, Thabit Zakaria, alisema: “Sisi
ndiyo mabingwa wa kihistoria wa Kombe la Mapinduzi.


“Kwa vyovyote itakavyokuwa, wakubali au wakatae Simba ndiyo vibonde wetu wa kihistoria, wanajua kuwa hawatuwezi na huo ndiyo uhalisia wenyewe.”



Naye Mkuu wa Idara ya Habari na Mawasiliano wa Simba, Ahmed Ally, aliliambia Spoti Xtra kuwa: “Mpira hauna historia na kama wanafikiria hivyo kuwa watatufunga kirahisi basi wamefeli, tunampiga Azam kama mtoto wetu.


“Sijaona beki wa kumzuia Sakho (Pape), hawana kipa wa kuzuia mashuti ya Kibu Denis, mapema tu wanakufa, waache kutegemea historia, hazina nafasi kwenye mpira.”

 

MASTAA SIMBA WALA KIAPO
Beki wa kati wa Simba, Henock Inonga Baka, amesema: “Ushindi ndio jambo la msingi kwetu, ni mchezo wa
fainali ambao si rahisi.


“Neno fainali tu linabadilisha maana nzima ya mechi, katika kuhakikisha tunafanya vizuri lazima tupambane, malengo yetu yanaifanya sisi kupambana kwa ajili ya kuyatimiza.”


Naye nahodha msaidizi wa kikosi hicho, Mohamed Hussein, alisema: “Azam ni timu ngumu na nzuri, hivyo
tunatarajia kupata upinzani mkubwa kutoka kwao, lakini mashabiki wa Simba wanatakiwa kutupa sapoti
ya kutosha ili kuhakikisha tunawapatia kile ambacho kinastahili ambacho ni ubingwa.”

 

AZAM YAJIANDAA NA PENALTI
Katika mazoezi ya mwisho ya Azam FC, wachezaji wa timu hiyo walikuwa wakipewa mbinu za kupiga penalti kwa ufundi jambo ambalo linaonesha wazi kwamba wanajiandaa na hatua hiyo kama ilivyokuwa dhidi ya Yanga.

Post a Comment

0 Comments
* Please Don't Spam Here. All the Comments are Reviewed by Admin.

Top Post Ad

Below Post Ad