Makarani sensa wabuni mbinu kuwakwepa wanaowapiga picha




Dar es Salaam. Katika kuwakwepa watu wanaowapiga picha na kuzirusha mitandaoni wakiwa wanakula, makarani wabuni mbinu kuwakwepwa watu hao.

 Agosti 23, 2022 wakati Sensa ya Watu na Makazi ilipoanza kulisambaa picha ikiwaonyesha makarani waki wanakunywa chai ilihali kuna wananchi wapo nyumbani wakiwasubiri kwa hamu wapite kuwahesabu.

Kitendo hicho kilitafsiriwa na baadhi ya watu ni kupoteza muda wa kazi waliyopewa waifanye huku wakijua kuna watu wanawasubiri wapite ili waende kwenye shughuli zao za utafutaji.

Akizungumza na Mwananchi Digital, leo Alhamisi Agosti 25, 2022 karani wa  Kata ya Kitunda, Jimbo la Ukonga, jijini Dar es Salaam, Yerusalemu Ntapwa amesema wanapoenda kula kwa sasa huwa wanavua vikoti hivyo na kuviweka kwenye mabegi.


Amesema wamelazimika kufanya hivyo kwa kuwa baadhi ya wananchi hawaelewi kwamba nao wana mahitaji kama ilivyo watu wengine ya kuhitaji kula muda ukifika.

"Ukiachilia kula yaani hata wakitukuta tumesimama sehemu tunapeana maelekezo ya namna bora ya kufanya kazi wanaanza kuturushia lawalama kwa tumewapuuza.

"Utawasikia wanasema tupo nyumbani tunawasubiri muda mrefu lakini mmekaa huku mnapiga soga hivyo jambo linalotufanya sasa tunapofanya haya tunalazimika tufiche kwanza vizibao vyetu kwa ajili ya usalama wetu,” amesema


Kutokana na kadhia hiyo, leo Alhamisi, Agosti 25, 2022, Waziri Mkuu wa Tanzania, Kassim Majaliwa amesema ipo haja ya kudhibiti tabia ya upotoshaji inayofanywa kwenye mitandao ya jamii.

"Zungumzeni na watu wenu wa Tehama ili wafuatilie. Pia picha zenye matumizi ya reflectors yasiyokuwa sahihi, ziachwe kusambazwa," amesema Majaliwa akitoa maelekezo kwa wakuu wa mikoa kwa njia ya mtandao na kuhudhuriwa na Nape Nnauye, Waziri wa Habari, Mawasiliano na Teknolojia ya Habari

Kuhusu hali ya kuhesabu watu, Yerusalem ambaye pia mmoja wa wasimamizi wa maeneo ya kata hiyo ya Kitunda, amesema ni mzuri  na mwitikio kwa wannchi umekuwa mkubwa.

Kwa upande wake, mwenyekiti serikali ya mtaa wa relini, Sospete Wankuru amesema licha ya makarani kujitahidi kufanya kazi changamoto imekuwa kwenye vishkwambi vyao kuishiwa chaji na kushauri ni vema wakapewa ‘power bank’ watembee nazo.


Hata hivyo, alitumia nafasi hiyo kuwaomba wananchi kuwasaidia kuchaji vifaa vyao pale wanapokuwa wanahitaji kufanya hivyo kwa kuwa kazi hiyo inafanywa kwa faida ya watanzania wote.

Baadhi ya wananchi akiwemo Tibeli Kalosi, mkazi wa Nyantira, amesema anashukuru yeye amekuta kaachiwa fomu ya kujaza kwa kuwa ni mtu wa kutoka saa 11 alfajiri na kurudi saa tano usiku.

"Kwa hili la kutuachia fomu naona wmefanya jambo jema kwa sisi tunaotoka asubuhi nakurudi usiku mnene, wasiwasi wangu upo tu kwenye namna ya kujaza sijui kama wote tutajaza kwa usahihi kama inavyotakiwa na nani ataturekebishia," amesema.

Neema Dastan, anayeishi Matembele ya Kivule amesema yeye jana aliporudi nyumbani dada yake alimwambia wameshajaza taarifa zake kwa kuwa naye huwa hashindi nyumbani.

Post a Comment

0 Comments
* Please Don't Spam Here. All the Comments are Reviewed by Admin.

Top Post Ad

Below Post Ad