Wanachama 384 CUF watimkia Chadema, Mbowe awapokea, Kambaya ndani…





JUMLA ya wanachama 384 wanachama wa Chama cha Wananchi CUF akiwamo aliyekuwa Mkurugenzi wa habari na uenezi wa chama hicho, Abdul Kambaya, wametangaza kujiunga na Chadema. Anaripoti Mwandishi Wetu …(endelea).

Hatua hiyo imejiri ikiwa ni siku chache tangu tarehe 23 Februari 2023, walipotangaza kujivua uanachama CUF kwa madai kuwa chama hicho kimepoteza mwelekeo na kumtuhumu Mwenyekiti Profesa Ibrahimu Lipumba kukiuka katiba ya chama hicho.


Akiwapokea wanachama hao leo tarehe 11 Machi 2023, Mwenyekiti wa Chadema, Freeman Mbowe amewakaribisha wanachama 384 wa CUF waliojiunga na chama hicho na kuwaeleza kuwa wao sasa ni sawa na mwanachama yeyote aliyemo ndani ya Chadema hata kama ni muasisi.

Amesema amefarijika kwamba wanachama hao wametoka ukanda wa Pwani – mwambao wa bahari ya Hindi kwa sababu awali Chadema ilijijenga zaidi bara na kukiachia CUF ukanda huo kutokana na imani yao ya kuamini katika ushirikiano.


“Kwa hiyo tukaona ukanda wa Pwani ni ukanda ambao ulikuwa umeshikwa na wenzetu wa CUF, tukaamini katika kushirikiana ndio maana tukaacha ukanda huo waukamate.

“Huko nyuma tuliamini sana katika kuunganisha vyama na Chadema hata katika katiba yetu kuna kipengele kinachozungumzia kwamba Chadema ni chama ambacho kitajitahidi kuunganisha vyama. Lakini azma yetu hii mara nyingi imekutana na misukosuko kwa sababu wenzetu mbele ya safari hukengeuka,” amesema.

Amesema kutokana na hali hiyo, Chadema wamedhamiria kuutekeleza wajibu huo kwa kuunganisha wananchi wenyewe kwamba badala ya kupoteza muda kupatana na vyama ambavyo havina dhamira moja.


Aidha, amewataka wanachama hao kuungana na ukanda wa Pwani katika kukiimarisha Chadema kuanzia ngazi ya mtaa, kitongoji hadi mkoa.

Amesema kiongozi yeyote wa Chadema atakayewakwamisha wanachama hao kufanya siasa kwa kuhofia kuondolewa kwenye nafasi yake, ataondolewa yeye.

Awali Katibu wa kamati hiyo, Shahada Issa amesema walifanya uamuzi wa kujivua uanachama wa CUF kutokana na chama hicho kukosa muelekeo.

Amesema walizungumza na vyama mbalimbali na baada ya kutafakari kwa kina waliona ni vyema kujiunga na Chadema ili kusongesha gurudumu kuelekea 2025.


Amesema baada ya kufanya uamuzi huo wanatarajia kuanza kuzunguka maeneo mbalimbali ili kujenga na kuendelea kukiimarisha chama hicho.
Tags

Post a Comment

0 Comments
* Please Don't Spam Here. All the Comments are Reviewed by Admin.

Top Post Ad

Below Post Ad