Kocha Stars amrudisha Fei Toto Young Africans



Kocha msaidizi wa timu ya taifa, Taifa Stars, Hemed Suleiman ‘Morocco’, amefichua jambo akisema amezungumza na kiungo Feisal Salum Fei Toto’ aliyeikaushia kambi ya Young Africans akimtaka arejee klabuni hapo, ili kujihakikishia namba katika kikosi cha Taifa Stars kwani watamtathmini kabla ya kuitwa tena baadae.

Fei yupo nje ya kikosi cha Young Africans tangu alipotangaza kuvunja mkataba na klabu hiyo na kuilipa Shilingi Milioni 112 zikiwamo za mishahara ya miezi mitatu, lakini klabu hiyo ikamgomea na kukimbilia Shirikisho la Soka Tanzania ‘TFF’ kupitia Kamati ya Sheria na Hadhi ya Wachezaji inayomtambua ni mali ya timu hiyo.

Hata hivyo, licha ya kutokuwa na timu tangu Desemba makocha wa Stars walimuita na kumjumuisha kiungo huyo kwenye kikosi kilichocheza mechi mbili za kuwania tiketi za Afcon dhidi ya Uganda na ukizuka mjadala juu ya kiwango chake, lakini Morocco amevunja ukimya na kuzungumza mipango ya benchi la timu hiyo kwa mchezaji huyo kwa mechi zijazo baada ya kuzungumza naye.


Morocco amesema kama makocha wataangalia namna ya kumtumia Fei kwa michezo iliyosalia kundini katika mchujo huo wa kwenda Ivory Coast na kuweka bayana kwamba alizungumza naye ili kumpa ushauri wa kipi cha kufanywa kwa sasa kulinda kiwango chake.

Morocco amesema kwa vile kuna miezi miwili mbele kabla ya Stars kucheza michezo ya mwisho ya Kundi F ikiwamo ya nyumbani dhidi ya Niger na ule ya kufungia dimba na vinara Algeria ambao wameshafuzu mapema kwenda ‘AFCON 2023’ kama itawezekana kumtumia kiungo huyo au la.


“Tuna michezo tena mwezi Juni hapa kuna miezi miwili chochote kinaweza kutokea, tutafanya tathmini na kama tutaridhika tutaona,” amesema kocha huyo kutoka visiwani Zanzibar.

Kocha huyo aliyewahi kuinoa Coastal Union na timu nyingine kwenye Ligi Kuu Bara amesema kama kocha alizungumza na Fei na kumpa kitu cha kufanya ikiwamo kukilinda kiwango chake, japo wenye mamlaka ndio wenye uamuzi wa mwisho.


“Kama kocha nimejaribu kuzungumza naye, lakini unajua haya mambo yanaendeshwa na mamlaka na watu wanaomsimamia Fei, hivyo ebu acha kwanza tuone kinachofuata, ila kuna mambo nimemshauri,” amesema Morocco
Tags

Post a Comment

0 Comments
* Please Don't Spam Here. All the Comments are Reviewed by Admin.

Top Post Ad

Below Post Ad