Le Mutuz kuagwa kesho Karimjee, kuzikwa Dodoma

Le Mutuz kuagwa kesho Karimjee, kuzikwa Dodoma


Mwili wa mmiliki wa Blogu ya Lemutuz, William Malecela maarufu ‘Le mutuz’ unatarajiwa kuagwa kesho Jumatatu Mei 15, 2023 kuanzia saa 5 asubuhi katika ukumbi wa Karimjee jijini hapa.

Le Mutuz ameaga dunia leo asubuhi Mei 14, 2023 baada ya kuugua kwa muda mfupi alfajiri na kupelekwa katika hospitali ya Mnazi Mmoja kisha Muhimbili.

Rafiki wa karibu wa Le Mutuz ambaye ametajwa na familia kusimamia msiba huo, Kinjekitile Kingunge (Kinje) ameiambia Mwananchi kwamba mpendwa wao atazikwa Dodoma kati ya Jumatano au Alhamisi.

"Tunamsubiri mzee (Malecela), leo jioni atakapowasili ndiyo itafahamika kama mpendwa wetu atapumzishwa kwenye nyumba yake ya milele Jumatano au Alhamisi.

"Lakini maziko yake yatafanyika Dodoma na kesho Jumatatu kuanzia saa tano asubuhi ataagwa kwenye viwanja vya Karimjee," amesema.

Akizungumzia kifo cha Le Mutuz, amesema kimekuwa cha ghafla na hadi jana jioni alikuwa mzima.

"Ndugu yetu alikuwa na matatizo ya moyo lakini alikuwa yuko vizuri tu, hadi jana usiku alikuwa mzima, ghafla leo alfajiri alijisikia vibaya akawahishwa hospitali ya Mnazi Mmoja ambako ni jirani na kwake.

"Kisha akahamishiwa Muhimbili, lakini ndiyo hivyo ametutoka," amesema Kinje.

Post a Comment

0 Comments
* Please Don't Spam Here. All the Comments are Reviewed by Admin.

Top Post Ad

Below Post Ad