Aanguka ghorofani akidhani mlango wa choo




Morogoro. Katika hali ya kushangaza, mwanaume aliyefahamika kwa jina moja la Rogan, ameanguka kutoka ghorofa ya tatu hadi ya pili katika Hoteli ya Cate iliyopo eneo la Kitungwa barabara ya Morogoro - Dar es Salaam, baada ya kupitia dirishani, huku akidhani ni mlango wa kuingia chooni.

Kaimu Kamanda wa Jeshi la Zimamoto na Uokoaji Mkoa wa Morogoro, Mkaguzi Emmanuel Ochieng, amethibitisha kwa kusema: "Tukio hilo limetokea leo alfajili na kwamba askari wa jeshi hilo walifika na kumuokoa mtu huyo ambaye alikuwa amekwama ghorofa ya pili."
Kamanda Ochieng amesema baada ya kupata taarifa kutoka kwa wahusika wa hotel hiyo, ilibainika kuwa mtu huyo alifika hotelini hapo jana akiwa na mke wake na walichukua chumba baadaye waliondoka na kurejea usiku.
Kwa mujibu wa kaimu bosi huyo wa jeshi hilo Mkoa wa Morogoro, ilipofika saa 11 alfajiri mke alihisi mume wake hayupo hivyo alianza kumtafuta chooni na baadaye aliona dirisha liko wazi, huku mume wake akiwa ananing'inia.
Kamanda Ochieng amesema baada ya kuokolewa, mtu huyo alipelekwa Hospitali ya Rufaa Mkoa wa Morogoro kwa matibabu, hata hivyo alionekana yuko kwenye hali ya ulevi kwa kuwa alikuwa hajitambui.
Kufuatia tukio hilo Kamanda Ochieng amewashauri watu wanaotaka kujenga majengo marefu kulishirikisha jeshi hilo katika usanifu michoro ili wataalamu wao waweze kushauri mambo muhimu ili kuepusha ajali na madhara yanayoweza kujitokeza.
"Sisi ni watu muhimu katika kushauri masuala ya ujenzi hasa wa majengo marefu, tunaweza kushauri ukubwa wa milango na madirisha na vitu vingine muhimu," amesema Ochieng.

Kwa upande wake Mganga Mkuu wa Moa wa Morogoro Dk Kusirye Ukio, amesema kwa sasa yuko nje ya hospitali hata hivyo ameahidi kufuatia taarifa hiyo.

Ni kweli nimesikia hiyo taarifa lakini kwa sasa sipo eneo la hospitali lakini ngoja nifuatilie kuona kama alifikishwa hapo hospitali na hali yake inavyoendelea, kisha nitatoa taarifa yenye uhakika," amesema Dk Ukio.

Post a Comment

0 Comments
* Please Don't Spam Here. All the Comments are Reviewed by Admin.

Top Post Ad

Below Post Ad