Kanisa la KKKT Nalo Latoa Msimamo wake Kuhusu Sakata la Bandari



Mkuu wa KKKT, Dk. Fredrick Shoo
KANISA la Kiinjili La Kilutheri Tanzania (KKKT), limemtaka Rais Samia Suluhu Hassan, kutumia busara katika kutafuta suluhu kuhusu sakata la uwekezaji bandarini, huku likisema linaendelea kumuunga mkono katika juhudi zake za kuleta maendeleo. Anaripoti Mwandishi Wetu, Arusha … (endelea).

Wito huo umetolewa leo tarehe 21 Agosti 2023 na Mkuu wa KKKT, Dk. Fredrick Shoo, akizungumza katika maadhimisho ya miaka 60 ya kanisa hilo, yaliyofanyika jijini Arusha.

“Najua katika jambo hili tumeingia katika kugawanyika kabisa, wengine wanatumia sababu za kidini, wengine wana maslahi yao ya kisiasa na kiuchumi, namshukuru Mungu amekujalia hekima katika hili kama kiongozi umekaa kimya,”

“Lakini nasema jambo hili linahitaji hekima kubwa ya kuliendea na sisi tunaendelea kukuombea kwa Mungu hekima itumike katika kuweza kuleta muafaka wa jambo hili pasipo wananchi kugawanyika na kutumika kama kitu cha kuchochea wananchi kwa watu wenye malengo mengine,” amesema Askofu Shoo.

Askofu Shoo amesema KKKT inaamini kwamba, maoni yaliyowasilishwa na viongozi wa dini katika kufanyia marekebisho ya mkataba wa ushirikiano wa kiserikali kati ya Serikali ya Tanzania na Imarati ya Dubai, kuhusu uendeshaji bandari, yatafanyiwa kazi.


“Naomba ieleweke wazi kwamba kanisa linaunga mkono uwekezaji, hatupingi uwekezaji. Mheshimiwa Rais tunajua wewe kwenye nia yako unataka wawekezaji, hata hivyo, jambo hili limekuwa na maoni mbalimbali, lakini sisi viongozi wa dini zote tulikuletea maoni yetu ukatusikiliza na ukaahidi utayapeleka kwa watalaamu na kufanyiwa kazi kwa uzito unaostahili na kwa maslahi mapana ya taifa,” amesema Askofu Shoo.

Askofu Shoo amesema “tunaimani na wewe Rais, tunakuamini na tunaamini ulisema taasisi na vyombo vyako vitafanyia kazi jambo hili unamaanisha hivyo.”

Katika hatua nyingine, Askofu Shoo amewataka viongozi wa dini na wanasiasa, wasitumie itikadi za dini kuwagawa wananchi.

“Umoja wa taifa letu la Tanzania, mshikamano ni muhimu kuliko mtu au kundi lolote, niwaombe viongozi wenzanguw a dini zote, wanasiasa waache misingi kuwagawa watu kwa misingi ya dini au misingi yoyote ya kisiasa au maslahi bianfsi, serikali yako kukemea kwa nguvu wale wanaonesha dalili za kutugawa kwa misingi ya itikadi zetu,” amesema Askofu Shoo.

Wakati KKKT likitoa msimamo wa kutaka mkataba ufanyiwe marekebisho, hivi karibuni Baraza la Maaskofu Katoliki (TEC), lilitoa waraka wake wakiupinga mkataba huo na kutaka Serikali iachane na mpango wa uwekezaji kwa madai kuwa hauna maslahi kwa taifa, pia wananchi wameupinga.

Post a Comment

0 Comments
* Please Don't Spam Here. All the Comments are Reviewed by Admin.

Top Post Ad

Below Post Ad