Maofisa Uhamiaji mbaroni mauji ya kijana Kakonko



Kakonko. Maofisa Uhamiaji wanne wanashikiliwa kwa mahojiano kuhusu kifo chenye utata cha kijana Enos Elias (20), mkazi wa Kijiji cha Ilabilo Wilaya ya Kakonko aliyekuwa akishikiliwa kwa mahojiano kuhusu uraia wake.

Kifo cha Enos ambaye enzi za uhai wake alikuwa akijishughulisha na kilimo na ujasiriamali kimegubikwa na utata baada ya kutoweka kwa siku kadhaa kabla ya mwili wake kukutwa ukiwa umezikwa na watu wasiofahamika katika pori la Kichacha Kijiji cha Chilambo kilometa kadhaa kutoka mjini Kakonko.

Kabla ya kutoweka na baadaye mwili wake kupatikana, kijana huyo aliwapigia simu ndugu zake kuwajulisha kuwa anashikiliwa na maofisa wa Jeshi la Uhamiaji Wilaya ya Kakonko baada ya kutiliwa mashaka uraia wake na kuomba atumiwe namba ya Kitambulisho cha Taifa (Nida) ya mama yake mzazi, Juliet Joseph ili aweze kuthibitisha uraia wake.

Taarifa zilizopatikana kutoka Kakonko na kuthibitishwa na Ofisa Uhamiaji Mkoa wa Kigoma, Novat Dawson zinasema maofisa wanne wa Uhamiaji Wilaya ya Kakonko wanashikiliwa kwa mahojiani kuhusu kifo hicho.


‘’Ni kweli wanashikiliwa tangu jana (Novemba 17, 2023)…lakini kwa maelezo zaidi kuhusu hilo wasiliana na Kamanda wa Polisi Mkoa wa Kigoma ndiye mwenye maelezo ya kutosha,’’ amesema Ofisa Uhamiaji huyo wa mkoa

Juhudi za kumpata Kamanda wa Polisi Mkoa wa Kigoma, Phillemon Makungu kuzungumzia sula hilo hazikufanikiwa baada ya simu yake kuita bila kupokelewa.

Maelezo ya familia

Akizungumza na waandishi wa habari nyumbani kwake Kijiji cha Ilabilo Wilaya ya Kakonko mkoani Kigoma, Juliet Joseph, mama mzazi wa kijana Enos amesema yeye, familia na jamii wanaamini kijana huyo amefikwa na mauti akiwa chini ya ulinzi wa maofisa wa vyombo na taasisi za Serikali.

Post a Comment

0 Comments
* Please Don't Spam Here. All the Comments are Reviewed by Admin.

Top Post Ad

Below Post Ad