Dk. Mpango: Sitakufa bali nitaishi




MAKAMU  wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dk. Philip Mpango amejitokeza leo Jumapili jijini Dodoma na kuwaelezea waumini wa Katoliki Parokia ya Mwenyeheri Maria Theresa Ledochowska kwamba alikuwa nje mwezi mzima kwa shughuli maalum. Anaripoti Faki Sosi…(endelea).

Akizungumza na waumini hao baada ya kushiriki Ibada katika kanisa hilo lililopo Kiwanja cha Ndege jijini Dodoma amesema mengi yamesemwa huku wengine walidhani yeye ni mzuka.


“Ahsante kwa kuniombea yamesemwa mengi si ndio?… na wengine bado wanasema mimi ni mzuka sasa wale mnaokumbuka mnaopenda kusoma bibilia labda niwakumbushe sehemu moja halafu nyinyi mtamalizia zaburi ya 118 aya ya 17 inasema sifakufa bali nitaishi “

Dk. Mpango ametanabaisha kuwa alikuwa nje kwa ajili ya majukumu maalam “Kwa hiyo mkae na amani niko salama nilikwenda nje kufanya shughuli maalam kwa takribani mwezi mmoja sijapungua hata kidogo”


Ametoa rai ya matumizi mazuri ya mitandao ya kijamii ili kuondoa taharuki.

“Mitandao ni mizuri lakini baadhi ya watu wanaitumia visivyo mnaona kilio cha baba inaumiza pia watu wengi …Tujitahidi sana kutumia mitandao ipasavyo kwa kumuogopa Mungu. Kwa hiyo wale waliokuwa wanatuma picha yangu na mishumaa pembeni … wengine wanasema mzee amekata moto bado kabisa kazi aliyonituma mungu kufanya sijaimaliza wakati utakapofika nitarejea kwa muumba wangu.”


Makamu wa Rais Dk. Philip Mpango akizungumza na kaka yake Padre Sebastian Mpango (kushoto) pamoja na Padre Emmanuel Mtambo (kulia) mara baada ya kushiriki Ibada ya Jumapili katika Kanisa Katoliki Parokia ya Mwenyeheri Maria Theresa Ledochowska Kiwanja cha Ndege Dodoma leo tarehe 10 Desemba 2023.
Awali uvumi wa kuwa Dk. Mpango kwamba yupo kwenye changamoto ya afya ulivuma mitandaoni sambamba na wanasiasa , wanaharakati na baadhi ya vyombo vya habari kuripoti mjadala alipo kiongozi huyo.


Awali Waziri Mkuu Kassim Majaliwa akihutubia kwenye siku ya kuenzi kumbukumbu ya Mwanasiasa mpigania uhuru Bibi Titi Mohammed Kibiti mkoani Pwani tarehe 3 Desemba aliwapa wananchi salama za Dk. Mpango.

” Mheheshimwa Dk Philipo Mpango ambaye yupo nje kwa majukumu achana na ule mtandao unaosema mambo ya ajabu ajabu yupo nje kwa majukumu anawatakia kila la heri watu wote mlioshiriki kwenye maadhimisho” alisema Waziri Mkuu Majaliwa

Makamu Mwenyekiti wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema) Tundu Lissu aliitaka Serikali ijitokeze ieleze alipo Dk. Mpango.


Tundu Lissu aliandika kwenye mtandoa wa ‘X’ (Twitter) juzi tarehe 8  Desemba ambapo aliandika taarifa mbili moja kwa lugha ya Kiingereza nyingine kwa Kiswahili zote zikiwa zinamaana moja.


“Hivi Serikali hii ilijifunza chochote juu ya kifo cha Magufuli mwaka juzi? Kifo au ugonjwa wa kiongozi mkuu wa nchi havifichiki! Kufichaficha kunaleta hisia mbaya za mchezo mchafu dhidi yake. Jisafisheni! Tuambieni aliko Makamu wa Rais Phillip Mpango sasa!” aliandika Lissu.

Ezekiel Kamwaga Mwandishi wa Habari mwandamizi kupitia ukurasa wake wa X aliandika “Kuna minong’ono mingi kuhusu alipo Makamu wa Rais Dk. Philip Mpango ..kutoonekana kwake kwa zaidi ya mwezi mmoja si jambo la kawaida . Na haitoshi kusema anaendelea na kazi huko aliko . Makamu wa Rais si jasusi kusema anatakiwa kufanya kazi zake kwa Clandestinely “usiri” Watanzania wana haki ya kujua alipo “.

Post a Comment

0 Comments
* Please Don't Spam Here. All the Comments are Reviewed by Admin.

Top Post Ad

Below Post Ad