Mchango ya Kumnunulia GARI Tundu Lissu Wafika Milioni 10



Mwanaharakati wa mitandaoni nchini Tanzania, Maria Sarungi ambaye anaendesha kampeni ya kumchangisha fedha za kununua gari jipya la Makamu Mwenyekiti wa Chadema (Bara), Tundu Lissu amesema michango hiyo imefika Sh10 milioni ndani ya saa 24.

Maria ametoa taarifa hiyo leo Jumapili Mei 19, 2024 saa 3 asubuhi kupitia ukurasa wake wa X (zamani Twitter).

Mei 17, 2024 Lissu alikabidhiwa na Polisi Mkoa wa Dodoma gari lake aina ya Toyota Landcruiser V8, VXR alilokuwa amepanda aliposhambuliwa kwa risasi na watu wasiojulikana miaka saba iliyopita.

Tukio hilo lilitokea Septemba 7, 2017, eneo la Area D, Dodoma wakati akitoka kushiriki vikao vya Bunge. Wakati huo alikuwa Mbunge wa Singida Mashariki (Chadema).

Mara baada ya kuwasili nyumbani kwake, kabla ya kushuka watu wasiojulikana waliokuwa wanamfuatilia walilishambulia gari hilo kwa risisi (upande alipokaa Lissu) na kumjeruhi vibaya sehemu mbalimbali ya mwili. Dereva wake alinusurika kwenye shambulizi hilo.

Baada ya tukio hiyo Lissu aliendelea na matibabu ndani ya nje ya nchi, huku gari hili likuwa kwenye yadi ya Polisi hadi juzi alipokwenda kulichukua, akisema atalitumia hadi litakapochoka na kisha ataliweka makumbusho, kauli iliyowaamsha wafuasi wake wakisema asilitumie, bali aliweke makumbusho na wao watachangia ununuzi wa gari jipya.

Michango yafikia Sh10 milioni

Mara tu baada ya tangazo hilo kuwekwa kupitia ukurasa wa sarangi na baadaye kwenye kurasa nyingine, michango ilianza kutolewa.

“Tumekusanya zaidi ya shilingi milioni 10 ndani ya saa 24, ni mwanzo mzuri, ila bado sana kukamilisha lengo letu la kumnunulia gari jipya na imara!” ameandika Maria Sarungi na kuongeza:


“Kutokana na urefu na uchovu wa safari, jana usiku @TunduALissu alishindwa kuweka mrejesho mapema, ila hana cha kusema zaidi ya kushukuru sana! Tuongeze juhudi kuchangia.”

Michango unaowasilishwa kupitia akaunti za Lissu, unalenga kumpatia gari jipya ili aondokane na kusudio la kutengeneza lile aliloshambuliwa nalo na kulitumia tena.

Jana Jumamosi Mei 18 2024, Lissu akizungumza na Mwananchi Digital amesema anautambua mchango huo na ameridhia.


“Huo mchango nautambua, watu wameniambia wanichangie ninunue gari, wakichanga hela ya kutosha nitanunua, hela isipotosha nitatengeneza hili,” amesema.

Baada ya kutangazwa kiasi kilichopatikana kupitia mitandao ya kijamii maoni mbalimbali yameibuka huku, makada wa chama hicho wakipeana moyo wa kuendelea kuchangia.

@clementc ameandika: “Polepole ndio mwendo. Hata ikituchukua mwaka kufikisha lengo so be it (na iwe). Tumeshaamua kama wananchi na tunajua umuhimu wa huu mchango, hamna wa kutuzuia.”

Naye @leocadia Njau ameshauri: “Tukipata watu milioni wakatoa buku2 (Sh2,000) kila mmoja gari imepatikana na chenji kubwa tu inabaki, naomba tuendelee kuhamasishana hizo jumbe (meseji) ziende hata kwenye viswaswadu yaani msg za kawaida zisambazwe watu wengi hawana mabando jamani.”

Meya wa zamani wa Ubungo, Boniface Jacob yeye ameandika kwenye ukurasa wake wa X: “Kwa niaba ya Boniyai Company Ltd, kupitia taasisi yetu Boniyai Foundation nitamchangia Shillingi million 2 Mheshimiwa Makamu mwenyekiti wa Chadema Tundu Lissu Kwa ajili ya kutengeneza gari yake au kununua gari mpya kwa jinsi Mh Lissu atakavyoona inafaa.”

Mjumbe wa Kamati Kuu ya Chadema, Gobdless Lema yeye aliweka picha ya Lissu kwenye ukurasa wake wa Instagram akizungumza baada ya kukabidhiwa gari lake kisha akaandika: “Hii gari haipaswi kutengenezwa hata kidogo. Inapaswa kubaki kama kumbukumbu, ili watoto/wajukuu wetu waweze kukumbuka sacrifice (sadaka) za wazazi wao katika kupigania demokrasia.”

Lema ambaye pia ni Mwenyekiti wa Chadema Kanda ya Kaskazini aliongeza: “Tunaweza kabisa kumtafutia Mh Lissu gari nyingine na imara kwa ku pledge only our very small donations (kwa kuahidi michango midogo) na gari hii ikabaki kuwa kumbukumbu ya majaribu tuliyopitia bila kukata tamaa wakati wa ujenzi wa demokrasia.”

Post a Comment

0 Comments
* Please Don't Spam Here. All the Comments are Reviewed by Admin.

Top Post Ad

Below Post Ad