Yanga Gari Limewaka, Vitalo Wafungwa Mdomo Mabao Manne Yawatosha

Yanga Gari Limewaka, Vitalo Wafungwa Mdomo Mabao Manne Yawatosha


YANGA imeendelea kuwapa raha mashabiki wake baada ya kuanza vyema michuano ya Ligi ya Mabingwa Afrika kwa ushindi mabao 4-0 dhidi ya Vital’O ya Burundi.

Katika mchezo huo wa awali uliopigwa kwenye Uwanja wa Azam Complex, Chamazi jijini Dar as Salaam, Yanga ilipata bao la kwanza dakika ya tano lililofungwa Na nyota mshambuliaji Mzimbabwe, Prince Dube kisha Clatous Chama kutupia la pili dakika ya 70 na Clement Mzize kuweka la tatu dakika ya 72, huku lile la tano likitupiwa na Aziz Ki kwa penalti baada ya kuangushwa ndani ya eneo la hatari la Vital’O.

MCHEZO WA MBINU

Mchezo huo ulianza kwa timu zote kucheza kwa tahadhari katika kipindi cha kwanza ambapo Yanga ambayo ilikuwa mgeni ilianza kwa kushambulia zaidi huku wenyeji, Vital’O wakizuia hadi waliporuhusu bao la utangulizi ndipo wakaanza kufunguka na kuifanya mechi kuleta ladha.

CHAMA AANZA KUTUPIA

Kocha wa Yanga, Miguel Gamondi alifanya mabadiliko matatu katika mchezo huo tofauti na mechi ya mwisho ya fainali ya Ngao ya Jamii ambayo timu hiyo iliibuka na ushindi wa mabao 4-1, Agosti 11, mwaka huu dhidi ya Azam FC.

Gamondi alimuanzisha kiungo mshambuliaji Chama ikiwa ni mechi yake ya kwanza kuanza ndani ya kikosi hicho tangu alipojiunga nacho msimu huu akitokea Simba.

Chama alianza akichukua nafasi ya kiungo mshambuliaji mwenzake, Pacome Zouzoua ambaye alianzia benchi baada ya mchezo wa fainali ya Ngao ya Jamii dhidi ya Azam FC kuanza kikosi cha kwanza.

Maeneo mengine ambayo Gamondi alifanya mabadiliko ni lile la beki wa kati ambapo nahodha Bakari Mwamnyeto alianza akichukua nafasi ya Dickson Job huku beki wa kushoto, Chadrack Boka ambaye pia alianza dhidi ya Azam FC akimpisha Nickson Kibabage.

DUBE HAKAMATIKI

Dube ameendelea kuonyesha makali ndani ya kikosi hicho baada ya bao lake kumfanya kufikisha manne tangu asajiliwe msimu huu akitokea Azam FC.

Nyota huyo alianza kufungua akauti katika michezo ya maandalizi ya msimu ‘pre Season’, Afrika Kusini timu hiyo ilipopata mwaliko ambapo alifunga mabao mawili.

Kisha Dube akaendeleza moto baada ya kuifungia timu hiyo bao moja katika ushindi wa mabao 4-1 dhidi ya Azam FC kwenye fainali ya Ngao ya Jamii huku likiwa ni la tatu Yanga.

YANGA NJIA NYEUPE

Kitendo cha Yanga kucheza michezo yote ya awali hapa nchini kutokana na Vital’O’ viwanja vyao kutokidhi vigezo kinaifanya timu hiyo kuwa na faida kubwa ya kutinga raundi ya pili ya michuano hiyo.

Ushindi huo kwa Yanga unaifanya kuhitaji sare katika mchezo wa marudiano utakaopigwa Agosti 24 jijini Dar es Salaam Ili kusonga raundi ya pili ya michuano hiyo.

Ikiwa Yanga itaitoa Vital’O katika michezo yote miwili itakutana na mshindi kati ya SC Villa ya Uganda au Commercial Bank ya Ethiopia kusaka tiketi ya kutinga makundi ya Ligi ya Mabingwa kama ambavyo ilifanya msimu uliopita kwa mara ya kwanza tangu iliposhiriki 1998.

VITAL’O WANYONGE

Kichapo kimeifanya Vital’O kuendeleza unyonge kwa Yanga kwani mara ya mwisho timu hizo zilipokutana ilichapwa pia mabao 2-0 katika michuano ya Kombe la Klabu Bingwa Afrika Mashariki na Kati maarufu kama Kagame 2008.

Kikosi cha Vital’O kilichoanza ni Hussein Ndayishimiye, Amedee Ndavyutse, Abdoul Karim Barandondera, Claude Masiri Luendo, Dieume Sisine Eboma, Kessy Jordan Nimbona, Claude Wakenge, Yakubu Uwimana, Autriche Nsanzamateka, Hamissi Harerimana, Prince Michael Musore.

Kikosi cha Yanga kilichoanza: Djigui Diarra, Yao Kouassi/ Denis Nkane, Nickson Kibabage, Ibrahim Hamad ‘Bacca’, Bakari Mwamnyeto, Khalid Aucho, Maxi Nzengeli/Pacome Zouzoua, Mudathir Yahya/Duke Abuya, Prince Dube/Clement Mzize, Stephane Aziz KI, Clatous Chama/Kennedy Musonda.

Post a Comment

0 Comments
* Please Don't Spam Here. All the Comments are Reviewed by Admin.

Top Post Ad

Below Post Ad